Katibu wa Itikadi na Uenezi Chama cha ACT - Wazalendo, Ndg. Ado Shaibu amedai sababu kubwa ya  chama chao kuonekana hakikubaliki na wanawake wengi ni kutokana na mazingira yasiyo rafiki ya kufanya siasa za upinzani yalivyo nchini na kwamba hayavutii wanawake.

Shaibu amesema kwamba uwezo wa kuvutia wanawake kujiunga na vyama vya upinzani ni changamoto kwa kuwa siasa hizo ni za mikiki mikiki na hiyo imepelekea kuwa tatizo la ki-nchi na siyo la ACT tuu.

Kiongozi huyo ameongeza kwamba licha ya kwamba mazingira kuwa ni magumu, wao ACT wamechukua takwimu hizo za Taasisi ya TWAWEZA kama changamoto na wataangalia mbinu zinazofaa ili kushawishi wanawake wengi kujiunga na vyama vya upinzani.

"Takwimu za TWAWEZA hatupingani nazo japokuwa zina changamoto, kwa hili la kukubalika na wanaume zaidi ya wanawake tumelichukua kama changamoto. 

"Tunatafuta mbinu za kuweza kushawishi wanawake wengi kujiunga. Unajua uwezo wa kuvutia wanawake wakaja kwenye siasa za upinzani ni changamoto sana. 

"Siasa za upinzani ni mikiki mikiki, mabavu, vitisho, mahakamani na kiuhalisia wanawake wana majukumu mengi sana ikiwepo kulea familia hivyo inakuwa changamoto kwao," amesema Shaibu.

"Lakini ukienda hata kwenye vyama vingine huwezi kukuta wanawake wengi kuliko wanaume, hata ukienda Kamati Kuu ya CHADEMA, hii ni kutokana na mazingira ya siasa zetu yalivyo, hii ni changamoto kwetu sote". Aliongeza

Pamoja na hayo Shaibu amevitaka vyama vingine kutopuuza utafiti huo wa TWAWEZA unapotolewa na badala yake waufanyie kazi na hata kama kuna mapungufu wajitahidi kutoa maoni ya maboresho na siyo kubeza.

Katika takwimu zilizotolewa na TWAWEZA wiki iliyopita zinaonyesha kuwa Chama cha ACT- Wazalendo kinakubalika na asilimia 24 ya wanawake huku wanaume wakiwa ni asilimia 40 tu.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: