Ahadi ya Chama Cha Mapinduzi ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 ya kutoa Sh. milioni 50 kwa kila kijiji na kila mtaa kwa sehemu za mijini, ambayo haijatekelezwa kwa miaka miwili mfululizo huenda ikaanza kutekelezwa baada ya jana Bunge kuitaka serikali kutoa taarifa bungeni kuhusu utekelezaji wake.

Akiwasilisha bungeni jijini Dodoma jana taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu makadirio ya bajeti ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa mwaka ujao wa fedha, Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo Jitu Soni, alisema pamoja na kwamba serikali iliahidi kutoa Sh. milioni 50 kwa kila kijiji, hadi sasa hakuna fedha yoyote iliyotolewa.

Alisema kuwa katika mwaka wa fedha 2016/17, serikali ilitenga Sh. bilioni 60 (Fungu 21) na katika mwaka huu wa fedha ilitenga kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya kufanya utafiti wa majaribio kwa baadhi ya mitaa, vijiji, kata na shehia kutekeleza mradi huo.

"Hata hivyo, fedha hizo zilizotengwa katika miaka yote, hakuna fedha yoyote iliyotolewa licha ya serikali kuahidi na kuweka utaratibu maalum kuhusu utoaji wa Sh. milioni 50 kwa kila kijiji kupitia Tamisemi," alisema.

"Kamati ingependa Bunge lako tukufu lipewe taarifa ya utekelezaji wa mradi huu ikiwamo 'Pilot Study' (utafiti wa majaribio) iliyofanyika," alisema.

Kiongozi huyo wa kamati pia alisema tathmini ya jumla ya mwenendo wa utoaji wa fedha za utekelezaji bajeti ya mwaka 2017/18 si wa kuridhisha kwa baadhi ya mafungu.

"Hadi kufikia Machi, mwaka huu, kati ya mafungu nane yaliyo chini ya wizara, ni miwili tu yaliyokuwa yamepokea fedha zaidi ya asilimia 60 ya bajeti zilizoidhinishwa na Bunge," alisema na kueleza zaidi:

"Kati ya mafungu 47 ya wizara mbalimbali yanayostahili kupata fedha za maendeleo ni mafungu 16 tu yamepata fedha zaidi ya asilimia 50."

Pia alisema mapato yatokanayo na ushuru wa usafirishaji wa fedha na bidhaa zinazotozwa ushuru wa bidhaa kama pombe kali yameshuka kwa asilimia 30.

"Kamati inaendelea kuishauri serikali kuhakikisha kwamba sera zake za kikodi kwa sekta zinazokua ziwe zina lengo la kulea na kuendeleza sekta hizo na si kukusanya kodi kiasi ambacho kinaathiri hata ukuaji wa sekta husika,"alisema.

Jitu pia alisema pamoja na michezo ya kubahatisha kukua kwa kasi na kuipatia serikali mapato, kamati yake inashauri kupanda kwa ada, tozo na kodi mbalimbali kwa kuwa kimsingi michezo hiyo si ya kiuzalishaji na imekuwa na madhara makubwa kwa jamii.

"Katika nchi za Afrika Mashariki, Tanzania inaongoza kwa kutoza kiwango cha chini kwenye mapato ghafi ya michezo ya kubahatisha kuliko nchi nyingine," alisema.

Alitolea mfano Kenya kuwa inatoza asilimia 35, Rwanda asilimia 13 na Uganda inatoza asilimia 20 ya mapato ghafi.

Alisema kamati inaitaka Bodi ya Michezo ya Kubahatisha (GBT) kusimamia kikamilifu sheria ili kuhakikisha kwamba wanaoshiriki katika michezo hiyo wawe wanafikia umri wa miaka 18.

Jitu pia alisema kamati yake inaishauri serikali kuhakikisha inalipa madeni yote ya watumishi, makandarasi na wazabuni yaliyohakikiwa.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: