Spika wa Bunge, Job Ndugai, ameitaka serikali kuhakikisha inatekeleza agizo lake la mwishoni mwa mwaka jana kuhusu kuwasilisha bungeni muswada wa sheria ya kuitangaza Dodoma kuwa makao makuu ya nchi vinginevyo atazuia kufanyika kwa mkutano ujao wa Bunge.

Novemba 17, mwaka jana, Spika Ndugai aliitaka serikali kuhakikisha muswada huo unasomwa kwa mara ya kwanza katika mkutano uliofuata uliofanyika kwa wiki mbili kuanzia Januari 30, lakini haikufanya hivyo.

Muda mfupi kabla ya kusitisha kwa muda kikao cha Bunge jijini Dodoma jana mchana, Spika Ndugai alikumbusha kuhusu agizo lake hilo na kumuonya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama kwamba hakuna muswada wowote wa serikali ambao utasomwa bungeni kabla ya kuwasilishwa kwa muswada wa kuitambua Dodoma kuwa makao makuu ya nchi.

"Hakuna muswada utakaosomwa hapa kwa mara ya kwanza kabla ya muswada huo. Na kwa maana hiyo, mkutano wa mwezi Oktoba hautafanyika," Spika Ndugai alisema.

Kiongozi huyo wa Bunge alitoa kauli hiyo baada ya Mbunge wa Iringa Mjini, Mch. Peter Msigwa (Chadema) kueleza bungeni jana kuwa mpango wa serikali kuhamia Dodoma haumo kwenye Mpango wa Taifa wa Maendeleo ya Miaka mitano 2015/6-2020/21.

Akichangia mjadala wa makadirio ya bajeti ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa mwaka ujao wa fedha, mbunge huyo alisema kuna mipango mingi imekuwa ikiibuliwa na kutekelezwa kwa fedha ambazo hazikuidhinishwa na Bunge.

Alisema mpango wa serikali kuhamishia shughuli zake Dodoma ni mfano mzuri kwa mipango inayotekelezwa bila kuidhinishwa na Bunge na haumo kwenye mpango mkuu wa serikali.

"Ndiyo maana leo tunahangaika kupata ofisi hapa Dodoma. Hatupingi serikali kuhamia Dodoma, lakini mpango huu Mheshimiwa Spika, haumo kwenye mpango wa serikali wa miaka mitano," Mch. Msigwa alisema.

Kutokana na kauli hiyo ya mbunge huyo, Spika Ndugai alisimama na kueleza kuwa suala la serikali kuhamia Dodoma limekuwa likiwekwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mpainduzi (CCM) tangu mwaka 1973.

Alisema kuna haja suala hilo liwe la kisheria, hivyo akamtaka Waziri Mhagama kuhakikisha anatekeleza agizo lake la kuwasilisha muswada huo bungeni vingine hatakubali muswada mwingine wowote kusomwa kwa mara ya kwanza ndani ya chombo hicho cha kutunga sheria.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: