Serikali imesema imefungua jalada la uchunguzi kuhusu mwanamke aliyejifungua sakafuni katika kituo cha polisi Mang’ula wilayani Kilombero katika Mkoa wa Morogoro,  Amina Mapunda.

Kauli hiyo imetolewa bungeni leo na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Yusuph Hamad Masauni alipotakiwa na Mwenyekiti wa Bunge, Andrew Chenge kutoa ufafanuzi wa Serikali kuhusiana na suala hilo.

“Tukio lililotokea huko Morogoro ni la ovyo kabisa na la kinyama na Serikali mnaweza kutoa kauli hapa na taifa likasikia,” amesema Chenge.

Akitoa kauli ya Serikali, Masauni amesema tayari jalada la uchunguzi limefunguliwa ili hatua kali za kisheria zichukuliwe.

“Tukio hilo lilimhusisha mume wa huyu mama ambaye alinunua kitanda cha wizi na polisi walipokwenda kwake wakakuta hicho kitanda cha wizi.

“Hivyo wakamkuta mke wake wakamchukua kwa ajili ya mahojiano, kitu ambacho hakikuwa sawa katika mazingira ya kawaida busara ingetumika.

“Hivyo serikali tumelichukulia kwa uzito suala hili na tunaendelea na uchunguzi halafu hatua kali zitachukuliwa,” amesema.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: