Na. Jeshi la Polisi.
Jeshi la Polisi nchini limefanikiwa kukamata Silaha mbalimbali na watuhumiwa 35 katika Oparesheni Maalum inayoendelea katika Ukanda wa mikoa ya  Kusini unaojumuisha mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma.

Akizungumza mkoani katika eneo la Kilambo mpakani mwa Tanzania na Msumbiji mkoani Mtwara, Mkuu wa Operesheni Maalum za Polisi, Naibu Kamishna wa Polisi Liberatus Sabas alisema kati ya watuhumiwa 35, wawili wamekabidhiwa Idara ya Uhamiaji kwa hatua zaidi, 16 wapo chini ya Upelelezi na 17 wapo chini ya uangalizi wa Polisi (Police Supervisee).

Sabas amezitaja Silaha zilizokamatwa kuwa ni pamoja na SMG mbili, Rifle mbili na Gobore moja ambapo amebainisha kuwa ufuatiliaji bado unaendelea ili kuwabaini wafadhili wa uhalifu hapa nchini.

“Kama nilivyosema kipindi kilichopita kuwa Operesheni hii ni endelevu na matokeo ndio kama haya hivyo hata wale waliokimbilia nchi jirani ya Msumbiji hawapo salama kwa kuwa hata kule operesheni zinaendelea na tunashirikiana na Jeshi la Polisi la nchi hiyo kuhakikisha kuwa wote wanakamatwa“. Alisema Sabas.

Aidha Kamanda Sabas amewataka wakazi wa mwambao wa mto Ruvuma kuendelea kutoa taarifa mapema mara tu waonapo watu wanaowatilia mashaka katika maeneo yao kwa kuwa uzoefu umeonyesha kuwa baadhi ya watuhumiwa wamekuwa wakitumia vipenyo vya mto huo na kufanya uhalifu kati ya nchi yetu na Msumbiji.

Pia amesema Operesheni hiyo inashirikisha vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama hivyo ametoa wito kwa raia wema kuendelea kutoa taarifa za siri ili kuendeleza amani na usalama hapa nchini.

Kufuatia mafanikio hayo, baadhi ya Wananchi katika mkoa wa Mtwara wamelipongeza Jeshi la Polisi kwa kazi kubwa inayofanya ya kuhakikisha kuwa wahalifu wanaosumbua wananchi wanakamatwa na kufikishwa mahakamani.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: