Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) inatarajia kujenga kituo kikubwa cha kupoozea umeme katika Jimbo la Kibamba baada ya Kituo cha Ubungo kuzidiwa.

Kauli hiyo imetolewa leo bungeni na Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu wakati akijibu swali la Mbunge wa Kibamba, John Mnyika ambaye alihoji serikali inachukua hatua gani kwa tatizo la kukatika katika umeme katika jimbo lake.

“Serikali kupitia Tanesco inajenga kituo kikubwa cha kupoozea umeme Kibamba kwa sababu kituo cha kusambaza umeme kutoka Ubungo kwenda Kibamba kilizidiwa.

“Kituo hicho kitajengwa baada ya kukamilika vituo vya Gongolamboto na sasa unaelekea Kibamba,” amesema Mgalu.

Naye Mbunge wa Viti Maalumu, Tunza Malapo (CCM), katika swali lake la msingi amehoji ni lini tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara litaisha katika Mkoa wa Mtwara.

Akijibu swali hilo, Mgalu amesema tatizo la kukatika umeme mara kwa mara katika mikoa ya Mtwara na Lindi inayopata umeme kutoka kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia kilichopo mkoani Mtwara kulitokana na kuharibika kwa mitambo ya kuzalisha umeme iliyochagizwa na uchakavu wa mitambo hiyo.

“Serikali kwa kushirikiana na Tanesco imechukua hatua mbalimbali ili kutatua tatizo la kukatika umeme katika mikoa hiyo,” amesema.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: