Naibu Mkurugenzi  wa Kampuni ya Simu Halotel, Trieu Thanh Binh (katikati) na baadhi ya wafanyakazi wa kampuni hiyo wakikabidhi msaada wa mahitaji mbalimbali ya kijamii  kwa baadhi ya wauguzi walipowatembelea watoto walio katika Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI) jana.

WATOTO wachanga wanaozaliwa na walio na umri chini ya miaka mitano huwa katika athari ya kuzaliwa au kupata magonjwa ambayo ni kuwa na vichwa maji, pamoja na mgongo wazi, ikiwa ni magonjwa ambayo huweza kuepukwa endapo tu jamii  nzima ya Watanzania wataweza kupatiwa elimu sahihi ya namna ya kuepuka au kuzuia magonjwa hayo na endapo kutabainika watoto wenye matatizo hayo jamii isiweze kuwaficha  kutokana na imani potofu.
Hayo yamebainishwa na daktari bingwa wa magonjwa ya upasuaji katika Taasisi ya Tiba ya  Mifupa Muhimbili (MOI), Laurent Lemeri Mchome, wakati akiongea na waandishi wa habari baada ya wafanyakazi wa kampuni ya simu ya Halotel walipowatembelea watoto wenye vichwa vikubwa na mgongo wazi pamoja na wazazi/walezi wao waliolazwa katika hiyo kwa ajili ya kuwapa mahitaji mbalimbali ya kijamii kama sehemu ya msaada wao kama wafanyakazi.

“Akiongea baada ya kukabidhiwa msaada huo, kwa niaba ya madaktari na wauguzi wodini hapo Dkt. Mchome amesema:
“Kila mwaka Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI) tumekuwa tukitoa matibabu kwa wagonjwa zaidi ya 350 nchi nzima  kupitia kampeni ya watoto wenye vichwa maji na mgongo wazi. Pia tumekuwa tukiweka kambi ya kutibu watoto kila mkoa kwa kila kanda nchini na changamoto kubwa ni kwamba jamii kubwa ya Watanzania hawana elimu ya kutosha kuhusu magonjwa haya kuwa yanatibiwa na watoto hupona kabisa”.

Wakati huohuo, akizungumza katika hafla hiyo, Naibu Mkurugenzi wa Kampuni ya Halotel, Trieu Thanh Binh, amesema kuwa katika kuhakikisha wanasaidia sekta hii ya afya nchini, wameona ni vyema kuwatembelea watoto hao na kujumuika nao siku hiyo ya leo kwa kuwapa misaada  ya kijamii ambayo  ni mwendelezo wa kampeni ya kusaidia jamii yenye uhitaji, ili waweze kuimarika katika afya zao wanapoendelea kupata matibabu wodini hapa. Hii ni pamoja ya kuonyesha upendo kwao na kutambua thamani yao katika jamii ya Watanzania.



Meneja Uhusiano wa  Kampuni ya Simu Halotel, Stella Pius, akikabidhi moja ya misaada ya mahitaji mbalimbali ya kijamii kwa mmoja wa wazazi wakati wafanyakazi wa kampuni hiyo walipowatembelea watoto walioko MOI.


“Tunatambua changamoto mbalimbali ambazo ziko katika kuwapa matibabu watoto wenye matatizo ya vichwa vikubwa na mgongo wazi wawapo wodini wakisubiri  kupata matibabu y upasuaji hivyo nitoe wito kwa taasisi zingine mbalimbali, makampuni na watu binafsi kuweza kujitolea na kuwasaidia mahitaji mbalimbali ikiwa ni katika kujali na kutambua thamani ya afya zao,” aliongeza Binh.

Kwa upande wa uongozi wa Taasisi ya MOI, Ofisa Uhusiano, Patrick Mvungi, alisema: “ Tumefarijika sana kwa kupokea msaada huu kutoka Kampuni ya simu ya Halotel na wafanyakazi wake, tunawashukuru sana kwa kuthamini afya za watoto hawa lakini pia kwa kuunga mkono jitihada za kuisaidia sekta ya afya nchini. Hii ni hatua mpya  na kubwa kwetu sisi katika kuimarisha ushirikiano wetu na Halotel kwa kiwango cha juu hasa katika kuboresha sekta ya afya kwa ujumla”.

Licha ya kampuni ya simu ya Halotel kupiga hatua kubwa katika kusambaza huduma za mawasiliano na kutoa huduma zenye ubora wa hali ya juu nchi nzima, kampuni hiyo imekuwa ikijihusisha na kutoa misaada mbalimbali kwa jamii ya Watanzania. Hii ni katika kuonyesha jinsi inavyothamini na kujali jamii ya Watanzania kwa nyanja mbalimbali, ikiwemo kuboresha sekta ya afya na elimu kama moja ya vipaumbele vya kampuni ya hiyo kwa maendeleo ya Watanzania na nchi kwa ujumla.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: