WABUNGE watatu kutoka Chama cha Wananchi (CUF) mikoa ya Lindi na Mtwara wamepongeza kasi ya utendaji kazi ya Rais John Pombe Magufuli katika kutatua kero za wananchi wa mikoa hiyo.

Wabunge hao Bw. Selemani Said Bungara (Kilwa Kusini), Bw. Zuberi Mohammed Kuchauka (Liwale) na Bw. Maftaha Abdallah Nachuma (Mtwara Mjini) walitoa pongezi hizo jana, (Jumatatu, Mei 21, 2018) wakati walipopewa nafasi ya kusalimia wananchi kwenye mikutano ya hadhara ambayo Waziri Mkuu alihutubia.

Akiwa wilayani Lindi, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa mara baada ya kuzindua kituo cha kuunganisha umeme wa gridi ya Taifa katika kijiji cha Mahumbika, aliwapa fursa wabunge wote alioambatana nao katika ziara hiyo maalum kwa ajili ya uzinduzi wa miundombinu ya nishati kwa mikoa ya Kusini.

Akizungumza na wananchi na viongozi wa taasisi mbalimbali mkoani humo waliohudhuria uzinduzi huo, Mbunge wa Kilwa Kusini, Bw. Bungara ambaye pia ni Mwenyekiti wa Wabunge wanaotoka Mkoa wa Lindi alisema analishukuru Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuisimamia vizuri Serikali ya CCM.

“Faida ya demokrasia ya vyama vingi ni kwamba CCM bila CUF, CCM hakuna na CUF bila CCM, kama ambavyo hakuna Simba bila Yanga wala hakuna Yanga bila Simba. Tuwe kitu kimoja tu, Kusini kwanza, vyama baadaye!” alisisitiza.

Alitumia fursa hiyo kumpongeza Waziri Mkuu kwa juhudi zake za kuwaunganisha wabunge wa mikoa ya Kusini bila kuwabagua au kujali itikadi zao.

Naye Mbunge wa Liwale, Bw. Kuchauka alisema: “Niwapongeze wewe Waziri Mkuu pamoja na Mheshimiwa Rais Magufuli kwa yale ambayo mnayasimamia na mnaamini kwamba yataleta ukombozi kwa wananchi wa Tanzania. Lazima nikiri kwamba wakati mnazindua sera ya uchumi wa viwanda, nilikuwa siamini katika hiyo sera yenu kwa sababu niliona ni moja ya mbinu zenu za kututenga sisi watu wa mikoa ya Kusini.”

“Niliona hivyo kwa sababu nilijiuliza unawezaje kuwa na uchumi wa viwanda wakati huna nishati ya uhakika ya umeme? Sasa nimeona mwanga kwamba mikoa ya Kusini nayo inaweza kushiriki kwenye uchumi wa viwanda,” alisema huku akishangiliwa.

Alisema hivi sasa hakuna asiyeona mambo yanayotekelezwa na Serikali ya awamu ya tano kwani dunia yote imekuwa kama kijiji na lolote linalofanywa na Mhe. Rais au Waziri Mkuu hakuna asiyejua. “Lolote analolifanya Mheshimiwa Rais au wewe Waziri Mkuu Watanzania wote watalijua, hakuna asiyeliona. Hivi sasa hakuna haja ya kubishana nani kafanya nini, jambo kubwa ni kuungana na tuangalie Tanzania yetu. Vyama vyote baadaye, Kusini kwanza,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mbunge wa Mtwara Mjini, Bw. Maftaha alisema mwaka 2006 baada ya kuhitimu kidato cha sita, alipangiwa afanye mafunzo ya ualimu kwa vitendo katika shule ya sekondari Mingoyo, eneo la Mnazi Mmoja lakini alitafuta nyumba ya kuishi yenye umeme hakupata.

“Wakati ule nyumba zenye umeme zilikuwa hazizidi hata 10, na kulikuwa na simba na wadudu wa kila aina. Leo nafarijika kuona kwa kasi ya ajabu, ninyi viongozi tuliowapa dhamana, mnatumia rasilmali za nchi hii, mnasambaza umeme kwa wananchi wa mikoa ya Kusini, na pale Mnazi Mmoja leo hii, umeme siyo tatizo tena.”

Wabunge wengine waliofuatana na Waziri Mkuu ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti na Mbunge wa Mtwara Vijijini, Bibi Hawa Ghasia; Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, Bi. Hamida Mohammed Abdallah (Viti Maalum). Mbunge wa Nachingwea, Bw. Hassan Elias Masala, Mbunge wa Nanyamba, Bw. Abdallah Dadi Chikota.

Waziri Mkuu alizuru pia mkoa wa Mtwara na kukagua ujenzi wa bandari, ukarabati wa mabomba ya kupokelea mafuta, matenki ya kuhifadhi mafuta, kuzindua upanuzi wa kituo cha kufua umeme kwa kutumia gesi asilia na kuzungumza na wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika uwanja wa bandari.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
Share To:

msumbanews

Post A Comment: