Mbunge wa Rombo (Chadema), Joseph Selasini amewaonya viongozi wa kisiasa kutolitumia Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) kwa shughuli za siasa.

Selasini ameshauri JWTZ kutumia kitengo chake cha upelelezi kulisaidia Jeshi la Polisi ambalo amedai limeshindwa kubaini matukio ya ajabu yanayoiaibisha nchi.

Hayo ameyasema leo Mei 14, 2018 bungeni jijini Dodoma wakati akichangia Bajeti ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ya mwaka 2017/18 huku akiwapongeza Waziri wa Wizara hiyo, Dk Hussein Mwinyi na Mkuu wa Majeshi, Venance Mabeyo kwa uongozi mzuri.

“Mimi nishauri tu, jeshi letu linaheshima katika majeshi ya Afrika, heshima yake inatokana na misingi yake na hili ni jeshi letu, ninaomba wanasiasa na viongozi wetu tusilichafue jeshi hili kama tulivyolichafua jeshi la polisi,” amesema Selasini na kuongeza:

“Leo katika nchi yetu, ikitokea ajali ya polisi, watu wanauliza wamekufa wangapi.”

Selasini amesema, “Hata katika operesheni  ya Ukuta (Umoja wa Kupambana na Udikteta Tanzania), wanajeshi walionekana wanafanya mazoezi, jeshi linalinda usalama wa mipaka, kwa nini tunalishughulisha na mambo yanayofanywa na polisi.”

Kuhusu upelelezi, Selasini amesema Mkuu wa Majeshi namshukuru atumie kitengo chake cha upelelezi.

“Ili haya matukio ya aibu, iko hofu, watu wanasema kuna maeneo nyeti nchini sasa yanalindwa na askari kutoka nchi hususan Rwanda, sasa hofu hiyo ya watu wasiojulikana inatia hofu.”
Share To:

msumbanews

Post A Comment: