Mama wa Msanii Wema Sepetu, Mariamu Sepetu, amebanwa mahakamani baada ya kuwasilisha nyaraka alizodai za matibabu ya msanii huyo India wakati ni nyaraka za kusafiria.

Tukio hilo limetokea leo Mei 29, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba wakati kesi matumizi ya dawa za kulevya inayomkabili Wema, ilipokuja kwa ajili ya kusikilizwa.

Wakili wa Serikali, Constantine Kakula alidai mahakamani kwamba kesi ilitakiwa kusikilizwa ushahidi wa upande wa utetezi lakini mshtakiwa wa kwanza, Wema hayupo ambapo mama Wema alidai msanii huyo ni mgonjwa yuko nchini India kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji na akawasilisha nyaraka alizodai kwamba zinathibitisha kuwa mgonjwa yuko kwenye matibabu.

Nyaraka hizo alizikabidhi kwa Wakili wa Serikali, Kakula ambaye alizikagua na kudai kwamba ni nyaraka za kusafiria ambapo alidai zilikuwa ni nyaraka za kusafiria na kumuomba mama Wema amuonyeshe mahali ilikoeleza kuhusu matibabu.

Mama Wema alijibu kwamba taarifa hizo atakuja kuzielezea Wakili wake Albert Msando ambapo Hakimu Simba alimfahamisha kwamba mahakama haiwezi kumsubiri hadi wakili wake aje.

Hata hivyo, Hakimu Simba alizichukua nyaraka hizo na kuzisoma kisha akasema nyaraka hizo ni tiketi na viambatanisho vya tiketi.

“Kesi itaendelea Juni 13, mwaka huu mshtakiwa aje na uthibitisho wa matibabu na kama hakutakuwa na uthibitisho, mahakama itatoa amri nyingine yoyote inayofaa,” alisema Hakimu Simba.

Mbali na Wema washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Angelina Msigwa  na Matrida  Abbas wanakabiliwa na kesi ya kutumia dawa za kulevya na kukutwa na kiwango kidogo cha dawa hizo.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: