Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema kasoro pekee ya utaratibu ulioanzishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kuwasikiliza wanawake na watoto ‘waliotelekezwa’ na waume zao ni kutokuwa na faragha kwa watoto.

Akizungumza leo Jumatano Aprili 11, 2018 wakati akihojiwa katika kipindi cha 360 kinachorushwa na televisheni ya Clouds, Ummy amesema kinachofanywa na Makonda kipo ndani ya sheria, hata watendaji wanaowasikiliza wanawake wametoka katika idara yake.

Amesema Wizara ya Afya inaunga mkono jitihada hizo, kwamba kasoro zilizojitokeza ni kwa baadhi ya wanawake waliotelekezwa kwenda na watoto na kutojali haki za kuwalinda katika hatua hizo za awali za mashtaka.

“Makonda amefanya kitu kizuri mwamko umekuwa mkubwa, ni sawa madawati yapo na ustawi wa jamii pia wapo lakini wengi wamekuwa wazito ila kwa sasa wameitikia wito kwakuwa yeye amewahimiza wanawake wenye matatizo hayo wafike kwake, kazi imekuwa nyepesi kwani hata wanaohudumia pale ni watu wetu wa Ustawi wa Jamii,” amesema Ummy.

Amesema kilichofanyika ni kama kuita kambi ambayo baadaye matokeo yatakayopatikana yatawanufaisha wanawake na ikiwa kutakuwa na ugumu kesi itakwenda mahakamani.

Hata hivyo, Ummy ametoa wito kwa wanawake wanaokwenda kutoa mashtaka yao kuhakikisha wanalinda haki za watoto wao kwa kutowaonyesha hadharani.

“Ninasema hili ni kosa la mwanamke mwenyewe, kwa mfano yule mtoto Mchina nimesikitika sana kule ni kumnyanyapaa amesambazwa mitandaoni kila mahali anazungumziwa, niwaombe Watanzania tujitahidi kuwalinda watoto hawa, tusisambaze picha zao kwa maslahi mazuri ya mtoto,” amesema Ummy. 
Share To:

msumbanews

Post A Comment: