Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imeendelea na msisitizo wa vituo vya Afya, Zahanati na Hospitali za serikali kuacha tabia ya kuuza dawa za kutibu malaria nchini na endapo mtoa huduma ataenda kinyume na hilo atachukuliwa hatua stahiki dhidi yake.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu wakati alipotembelea Zahanati ya Mwandiga iliyopo wilayani Kigoma Mkoa wa Kigoma katika akiwa anangalia hali ya matibabu dhidi ya malaria wilayani humo kuelekea kilele cha siku ya Malaria Duniani.

"Nawaagiza waganga wakuu wa Mikoa na Wilaya kuweka matangazo yanayooonyesha kipimo cha haraka cha Malaria, dawa za kutibu Malaria ya mseto na sindano ya kutibu malaria kali ni bure kwenye kila zahanati, kituo cha afya na hospitali ya serikali", amesema Waziri Ummy.

Aidha, Waziri Ummy amewataka waganga wakuu wa vituo ngazi za zahanati na waganga wakuu wa wilaya waweke namba zao za simu kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini ili kuwasaidia Watanzania kutoa malalamiko yao pindi wanapopatiwa huduma ambazo za hazikidhi viwango ili kubendelea kuboresha huduma za afya nchini.

Waziri Ummy amesema kuwa katika kujikinga na Malaria wananchi wanatakiwa kutumia vyandarua vyenye dawa, kusafisha mazingira na kuondoa mazalia ya mbu waenezao ugonjwa huo kwani kinga ni bora kuliko tiba.

Sambamba na hilo Waziri Ummy ametoa vyandarua vyenye dawa ya kukinga dhidi ya Malaria katika kijiji cha Mwandiga ili kuendelea na juhudi za kutokomeza Malaria nchini katika kuelekea siku ya Malaria Duniani.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: