Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknlojia Profesa Joyce Ndalichako amelitaka shirikisho la Mameneja na Wamiliki wa Shule nchini –TAMONGSCO kuwa na mtazamo chanya wanapotekekeleza majukumu yao ikiwa ni pamoja na kuelewa kuwa kila Jambo linautaratibu wake katika kulitekeleza.

Waziri Ndalichako ameyasema hayo leo mkoani Dodoma wakati akifungua mkutano Mkuu wa Shirikisho hilo ambapo amesisitiza kuwa Elimu ni kitu muhimu na hakiwezi kuendeshwa bila kufuata utaratibu, kusisitiza kuwa hata uendeshaji wa shule una taratibu zake.

Profesa Ndalichako aliwaeleza wajumbe wa mkutano huo kuwa Serikali haiwezi kuweka vikwazo na vizuizi kwa wadau wake wa Elimu, kwa kuwa lengo ni kuhakikisha Elimu bora inatolewa kwa manufaa ya Taifa.
“Hata siku moja Serikali haiwezi kuweka vikwazo na vizuizi kwa wadau ambao kwa namna moja ama nyingine wamekuwa mstari wa mbele kuunga mkono  juhudi zinazofanywa na serikali, Pia Serikali inatambua thamani na mchango unaotolewa na sekta binafsi katika Elimu,
 “Hivyo sioni kuwa  ni sahihi kwenu nyinyi TAMONGSCO kuja na kauli mbiu inayosema kuwa  “ Kwa nini vikwazo na vizuizi katika shule na Taasisi zisizo za Serikali,”alisema Waziri Ndalichako.
Waziri Ndalichako pia amewataka Mameneja na Wamiliki hao wa shule kuwa wazalendo kwa kutoa kipaumbele katika kuajiri walimu wa Kitanzania, kabla ya kufikiria wageni.
Amesema ili kuunga mkono kauli mbiu ya Serikali ya awamu ya tano ya kujenga uchumi wa viwanda ni vyema wawekezaji wakawekeza zaidi kwenye eneo la ufundi stadi, ikiwa ni pamoja na mafunzo yanayotolewa kuendana na soko la ajira.
Kwa upande wao TAMONGSCO wameeleza kuwa lengo la mkutano wao ni kujadiliana kwa pamoja mafanikio na changamoto mbalimbali zilizopo katika sekta ya Elimu ili kuzipatia ufumbuzi wa pamoja.

Imetolewa na:
Kitengo Cha Mawasiliano Serikalini,
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA.
04/04/2018



Share To:

msumbanews

Post A Comment: