Mbunge wa jimbo la Singida Mashariki, mheshimiwa Tundu Antipasu Lissu jana amemjibu Spika wa bunge mheshimiwa Job Ndugai, kutokana na kauli ya spika huyo aliyoita hapo juzi, akijibu swali la mbunge wa Arusha Mjini Godbless Lema juu ya sababu kwanini bunge mpaka halijagharamia matibabu yake.
Lissu ambaye yupo nchini Ubeligiji kwa matibabu, alishambuliwa kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana, nyumbani kwake mjini Dodoma hapo septemba 7, 2017 majira ya mchana, ambapo mpaka sasa bunge na serikali hawajagharamia matibabu yake.
Hapo jana Spika wa bunge la jamhuri ya muungano wa Tanzania, alisema kuwa bunge halijagharamia matibabu ya mbunge huyo, kwa sababu kuna vigezo bado havijafuatwa ikiwa ni pamoja na kibali cha Rais, kibali cha wizara ya afya na kibali toka hospitali ya taifa ya Muhumbili kama utaratibu ulivyo.
Tundu Lissu afafanua kuwa utaratibu wa matibabu ya mbunge yeyote wa bunge la jamhuri, umewekwa na sheria ya bunge iitwayo Sheria ya Uendeshaji wa bunge ya mwaka 2008. Na katika kifungu cha 24 Kipengele cha kwanza cha Sheria hiyo kinasema matibabu ya mbunge yatagharamiwa na bunge ndani na nje ya Tanzania.
“Kwa utaratibu wa sasa ulivyo, bunge linalipia gharama za tiba na gharama za kujikimu za mbunge na ndugu anayemuuguza.
Sheria ya uendeshaji wa bunge haijaweka masharti anayoyazungumzia Spika Ndugai. Hakuna kifungu chochote kinachozungumzia kibali cha Muhimbili au cha Magufuli.” Amesema Lissu.
Mheshimiwa huyo ameongezea kuwa kauli ya Spika Ndugai inathibitisha jinsi ambavyo bunge limepoteza mamlaka na hadhi yake chini ya uongozi wake na masuala ambayo sheria haijampa Rais mamlaka, Spika Ndugai ameweza kuyakabidhi kwa Rais Magufuli kinyume na taratibu.
“Kauli hiyo ni uthibitisho pia wa jinsi ambavyo Bunge linaendeshwa bila kufuata sheria, kwa chuki na upendeleo wa kisiasa chini ya uongozi wa Spika Ndugai.
“Yeye amekwenda India mara nyingi kutibiwa kabla na baada ya kuwa Spika kwa gharama za bunge. Mimi mbaya wao niliyepigwa risasi nikiwa nahudhuria vikao vya Bunge ninakataliwa matibabu kwa sababu zisizokuwa na msingi wowote.” Amesema Lissu.
Mhe Lissu amesisitiza kuwa sio kweli kwamba hakufuata utaratibu uliowekwa na sheria. Kwani katika mazingira ya jaribio la mauaji dhidi yake, utaratibu pekee uliokuwa unawezekana ulikuwa ni kumhamisha nchini kwa dharura.
“Nilikuwa nimeumizwa vibaya, mifupa imevunjwa kila mahali, nimepoteza damu nyingi na risasi zimejaa tumboni.
“Kusema nisubiri kibali cha Bunge au cha Muhimbili au cha Magufuli ilikuwa ni kunitakia kifo cha wazi. Pengine ndicho Spika Ndugai na wakubwa wake walichokitaka. Mungu aliwakatalia, sasa wamenuna.” Ameongezea Lissu.
Amesema suala kibali sio kweli, kwamba hakuwa na kibali, kwa sababu alipata kibali cha kupelekwa hospitali ya Nairobi nchini Kenya na uamuzi wa kupelekwa huko ulifanywa kwenye kikao kilichofanyika hospitali ya mkoa wa Dodoma na Spika Ndugai na Naibu wake, katibu wa bunge Dr Tom Kashilila, Waziri wa afya Ummy Mwalimu na viongozi wengine wa kisiasa akiwemo Mbowe walikuwepo kwenye kikao hicho.
Hata hivyo, mbunge huyo amekana kuhusu taarifa za kupatiwa matibabu na serikali ya Ujerumani na kusema gharama za matibabu yake zinaghamikiwa na serikali ya nchini Ubeligiji.
“Spika Ndugai ametoa kauli hii kwa sababu ukweli ni kwamba hajui na hajawahi kujua natibiwaje. Angeuliza angepewa taarifa sahihi, lakini hajawahi kuuliza.
“Ukweli ni huu. Gharama zote za tiba zinagharamiwa na bima ya afya ya Ubelgiji ambayo mimi na mke wangu tulijiunga mara baada ya kufika hapa. Gharama za bima, ambazo kwa hapa sio kubwa sana, nimelipia mwenyewe.” Amesema Lissu
Aidha, Lissu ameleeza kuhusu gharama zingine kama kujikimu, kupanga nyumba, chakula, usafiri, n.k, kuwa ni michango ya wasamaria wema Watanzania na wasio watanzania, ambao hata hajawahi kuwaona au kuwafahamu ndio wamemuwezesha yeye na familia yake kuweza kukaa huko Ubelgiji kwa miezi yote ambayo anapata matibabu.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: