Dodoma, April 13, 2018:
Serikali imefafanua hatua zilizochukuliwa kuhakikisha Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) linafaidika na kampuni ya ubia ya StarMedia, huku ikisisitiza kuwa uongozi wa sasa chini ya Rais John Pombe Magufuli umefanya mageuzi makubwa na ya kihistoria katika kuwawezesha wajasiriamali wadogo na wa kati.

Wakizungumza mjini hapa jana katika mfululizo wa mawaziri kufafanua utekelezaji wa hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Dkt. Harrison Mwakyembe, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Mhe. Charles Mwijage, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, wamesisitiza ripoti ya CAG ni nyenzo muhimu kwao.

Dkt. Mwakyembe: TBC Sasa Kufaidika na StarMedia
Akizungumzia hoja ya CAG kuhusu mkataba wa StarMedia, Waziri Mwakyembe amewaambia waandishi wa habari kuwa changamoto kubwa iliyosababisha kampuni hiyo kutozalisha faida kwa miaka saba sasa ni udhaifu katika uendeshaji wa kampuni na baadhi ya watendaji wa zamani wa TBC waliotarajiwa kusimamia maslahi ya Taifa kususa, kujiuzulu na kuuacha uendeshaji chini ya wabia kutoka China.

Hata hivyo Waziri Mwakyembe ameongeza kuwa baada ya Serikali kumwagiza CAG kufanya ukaguzi ikiwemo pia yeye binafsi Kuunda Kamati Maalum ya Waziri kuchunguza mkataba wa StarMedia, sasa makubaliano yamefikiwa ili kuondoa dosari zote.

“Baada ya majadiliano ya muda mrefu na wenzetu wa StarTimes Group (kampuni mama yenye hisa nyingi katika ubia wa StarMedia), wenzetu hatimaye wamekubali taarifa ya CAG na mapendekezo yake yote,” alisema Waziri Mwakyembe.

Aliyataja baadhi ya makubaliano yaliyosainiwa ili kuigeuza StarMedia kujiendesha kwa ufanisi zaidi kuwa ni pamoja na: kufanyiakazi hoja zote za CAG, kuongeza wafanyakazi zaidi wa Kitanzania katika menejimenti, uwazi zaidi katika uendeshaji wa kampuni na kuanzia sasa Bodi ya ubia inayoongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa TBC kuwa ndio chombo cha juu cha uamuzi badala ya kusubiriwa maelekezo kutoka Beijing, China.

Aidha, Waziri Mwakyembe ameeleza kuwa, kwa kuwa kampuni hiyo haikuwa kutoa gawio kwa wanahisa wake, kuanzia mwaka huu, wakati kasoro zote zilizobainishwa na CAG na Kamati ya Waziri zikifanyiwakazi, StarMedia itatoa ruzuku ya Shilingi Bilioni tatu (3) kwa TBC.

“Kwa niaba ya Serikali, Wizara yangu itafuatilia kwa karibu utekelezaji na haitasita kuchukua hatua kali za kisheria na kinidhamu kwa mtendaji wa upande wowote atakayekuwa kikwazo katika uendeshaji wa kampuni,” alisema.

Waziri Mwijage: Tumeongeza Bajeti Kuinua Wajasiriamali
Kwa upande wake, Waziri Mwijage, akifafanua hoja mbalimbali zilizoelekezwa katika Wizara yake alisema ameshaagiza hatua za haraka zichukuliwe kwa taasisi zote zilizo chini ya wizara yake kutekeleza hoja mahsusi za CAG. 

Kwa upande wa hoja ya mchango mdogo wa Sekta ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati nchini, Waziri Mwijage amefafanua kuwa wakati lengo kuu ni ifikapo 2025 sekta hiyo kuchangia Pato la Taifa kwa asilimia 40, tayari kwa ushirikiano wa Serikali na sekta binafsi, inachangia asilimia 35, ambazo ni kubwa ikilinganishwa na nchi jirani.

“Kwa kulinganisha mchango wa sekta hii kwa Tanzania katika pato la taifa na nchi nyingine bado nchi yetu inafanya vizuri. Kwa Kenya sekta hiyo inachangia takribani asilimia 25; Uganda asilimia 20; Afrika ya Kusini asilimia 36; India asilimia 40 na Malaysia 40,” alisema.

Aidha, Waziri Mwijage amesisitiza kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imefanya mageuzi makubwa katika utoaji wa mtaji kwa Mfuko wa Kuendeleza Wajasiriamali (NEDF) na Shirika la Kuendeleza Viwanda Vidogo (SIDO) ambapo mwaka jana Mfuko huo ulipewa Bajeti ya Shilingi bilioni tano (5), mwaka huu Bajeti iliongezwa hadi shilingi bilioni saba (7.8).

Bajeti ya SIDO imeongezeka mpaka shilingi bilioni 26.8; kiasi ambacho ni cha kihistoria kwani hakijapata kutolewa na Serikali kabla ya kuingia Awamu ya Tano.

“Kama CAG alivyobaini, sekta hii ni uti wa mgongo wa Taifa kulingana na uchangiaji wake katika pato la Taifa na ajira. Kutokana na nafasi ya sekta hii katika kujenga taifa la uchumi wa kati, ni mpango wa Wizara kuendelea kuiongezea rasilimali zaidi,” alisema.

Katika mfululizo wa Mawaziri wa Serikali ya Awamu ya Tano kufafanua utekelezaji wa hoja mbalimbali za CAG, Jumatatu ijayo itakuwa zamu ya Wizara ya Kilimo na Wizara ya Mifugo.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: