MWANDISHI: INNOCENT MAKAUKI

INSTAGRAM: Makeynovels_tz
MOVIE SCRIPTS/ BOOKING YA KITABU: 0622088300

Inaendelea ilipoishia toleo lilopita.....

SEHEMU YA SITA

Job akapiga hatua kadhaa na tayari akawa yuko upande wa pili wa gari na kuanza kugeuka taratibu wakati huu akijua fika huyu mtu hakua na nia ya kumdhuru bali kuna kitu kingine zaidi alichoitiwa kuhusu majibu aliyoahidiwa.

Aligeuka na akawa anamuona moja kwa moja mtu huyu aliyekua bado ameishikilia bastola yake vizuri bila kujitingisha kwa namna yoyote.

Alikua ni mtu wa makamo kwa muonekano wa miaka kati ya arobaini hadi hamsini. Kivinginevyo angekua na umri mkubwa zaidi kulingana na muonekano wake.

Mrefu wa kadiri ya futi sita unusu, mweusi kama watu wa kanda ya ziwa na mpana wa mwili ila zaidi alitisha kwa jeraha kubwa lililochukua sehemu kubwa ya upande wa uso wa kulia mithili ya mwanajeshi wa kivita aliyeparuzwa na risasi iliyotarajiwa kutawanya ubongo wake au aliyepigwa panga butu na askari wa kundi lisilo na huruma la boko haram.

Bila kupoteza muda akafungua mlango wa gari wa upande wake akiwa ameilenga bastola yake vizuri alipo Job akihakikisha hakuna mchezo wowote mchafu akachukua file la kijani lililokua kwenye dashboard na kulitupa juu ya bonnet huku akimwambia Job "fungua hilo file".

Job akimwangalia usoni mwenyeji wake huyu akapeleka mkono wake wa kulia na kuliburuza file taratibu na kulisogeza karibu yake.

 Juu liliandikwa -TOP SECRET-kwa maandishi meusi yaliyokolezewa wino. Hatua iliyofuata akafungua ndani ambako ilionekana ni file iliyojumuisha karatasi nyeupe kama kumi kwa makadirio ya palepale zilizofungwa vizuri na uzi wa file. Kwenye ukurasa wa kwanza hapakuandikwa maneno mengi bali katikati ya ukurasa paliandikwa -OPERATION D.O.A- ambayo hayakua maneno mapya kwa Job akiwa ameshatajiwa mara kadhaa katika upelelezi wake, operesheni iliyohusishwa na orodha kubwa ya maangamizi wakiwemo viongozi wakubwa serikalini na matajiri wakubwa nchini.

Orodha ambayo Job ameifanyia kazi kwa muda wote wa miezi mitatu lakini alichoweza kukipata ni majina kadhaa tena ya wale waliokwisha angamia akiwemo Mkurugenzi mkuu wa kampuni kubwa ya usafirishaji wa majini Broca Shipping Company aliyepigwa risasi nyumbani kwake siku moja baada ya kutekwa kwa meli yake iliyosemekana kusheni mzigo wa silaha za kivita. Mwingine aliyekua.....

Itaendelea kesho
Share To:

msumbanews

Post A Comment: