Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na wageni mbalimbali kutoka ndani na nje ya Nchi kabla ya kuzindua rasmi Taasisi hiyo isiyo ya Kiserikali ya Jakaya Mrisho Kikwete(JMKF) Ikulu jijini Dar es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akipigiwa makofi mara baada ya kumaliza kusoma hotuba yake na kuizindua rasmi Taasisi hiyo isiyo ya Kiserikali ya Jakaya Mrisho Kikwete(JMKF) Ikulu jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Taasisi hiyo ya (JKMF) Rais Mstaafu wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akizungumza kabla ya uzinduzi wa Taasisi hiyo Ikulu jijini Dar es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimpongeza Mwenyekiti wa Taasisi hiyo ya (JKMF) Rais Mstaafu wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete mara baada ya kuizindua.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akijadiliana jambo na Mwenyekiti wa Taasisi hiyo ya (JKMF) Rais Mstaafu wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete mara baada ya kuizindua. PICHA NA IKULU

*Azungumzia mambo makubwa ambayo aliyafanya kwenye utawala wake ambayo yatakumbukwa
*Azindua rasmi Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete Foundation,aahdi Serikali kutoa ushirikiano mkubwa
*Alezea Kikwete alivyosababisha awe Rais wa Awamu ya Tano, Kikwete azungumzia malengo ya taasisi

Na Said Mwishehe, Globu ya Jamii.

RAIS Dk. John Magufuli amesema kwa kazi kubwa ambayo imefanywa na Rais mstaafu Jakaya Kikwete kwenye uongozi wake kuna mambo makubwa ya maendeleo katika nchi yetu huku akitanguliza uzalendo mkubwa Watanzania wanamkumbuka na wataendelea kukumbuka watake wasitake.

Pia ametumia nafasi hiyo kutoa shukrani zake za dhati kwa Rais mstaafu Kikwete kwani ndio amesababisha awe Rais wa Serikali ya Awamu ya Tano huku akitumia nafasi hiyo kuahidi kuwa atahakikisha Serikali yake itashirikana na Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete inayofahamika kwa Jakaya Mrisho Kikwete Foundation (JMKF)ambayo ameizindua rasmi leo Ikulu jijini Dar es Salaam.

"Mzee wangu Kikwete naomba niseme kutoka moyoni wakati wa uongozi wako umefanya mambo makubwa ya kuleta maendeleo kwa ajili ya nchi yetu ya Tanzanania.Kuna miradi mikubwa ya maendeleo ambayo ameifanya na imeacha alama ambayo itatufanya watanzania tumkumbuke.Kwa kazi ambayo umeifanya kwa uzalendo mkubwa ndani ya nchi yetu Watanzania tunakukumbuka na tutaendelea kukumbuka watake wasitake,"amesema Rais Dk.Magufuli.

Ametaja ipo mifano mingi hai ya mambo ambayo ameyafanya Rais mstaafu Kikwete kwenye Serikali ya Awamu ya nne na baadhi ya miradi hiyo lipo  la ujenzi wa bomba la gesi kutoka mkoani Mtwara hadi Dar es Salaam, ujenzi wa miundombinu ya barabara nchi nzima, ujenzi wa miradi ya maji , umeme na kuimarisha sekta muhimu za afya, kilimo na vijana.

"Rais mstaafu Kikwete alilitumikia Taifa la Tanzania kwa uadilifu mkubwa.Tabia ya binadamu wamekuwa na kawaida ya kumsifu mtu baada ya kufa na kusema pengo halitazibika wakati si kweli kwani kama ni nafasi ya uongozi inaweza kujazwa wakati huohuo.Kwa Rais mstaafu na mzee wangu Kikwete naomba nikusifu ukiwa hai tena upo mbele yangu unatabasamu.Umefanya kazi kubwa ya kizalendo kwa ajili ya nchi yetu ya Tanzania na unastahili sifa na shukrani kutokana na mchango wao wa kuleta maendeleo kwenye nafasi mbalimbali.

"Ulipokuwa Rais wa Tanzania umefanya mambo makubwa zaidi kwa ajili ya nchi yetu. Katika utawala wako umefanikisha ujenzi wa shule za sekondari za kata , ujenzi wa Hospitali ya Mloganzila na miradi mingine mikubwa ambayo umeifanya na sote ni mashahidi kwa yale ambayo umeyafanya,"amesisitiza Rais Dk.Magufuli na kuongeza mbali ya kuwa Rais mzee Kikwete ameshika nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya Bara la Afrika na nchi za ulaya na Dunia kwa ujumla na kote huko ametoa mchango mkubwa wa kuleta maendeleo .

Rais Magufuli amesema uzalendo wa mzee Kikwete kwa nchi yake umemfanya hata baada ya kustaafu kuamua kuanzisha taasisi ambayo leo amezindua rasmi na vipaumbele vya taasisi hiyo havina tofauti na vile ambavyo anavitekeleza kwenye Serikali yake , hivyo ameahidi kumpa ushirikiana mkubwa kufanikisha malengo hayo na kuomba wadau wengine wakiwamo mabalozi nao kuunga mkono kazi za taasisi hiyo.

"Mzee Kikwete ameiga mfano wa watangulizi wake kuanzia Mwalim Nyerere, Mzee Mwinyi na mzee Mkapa ambao nao baada ya kustaafu kuongoza nchi waliamua kuendelea kutoa mchango wao wa kulitumikia taifa na hivyo kitendo cha Rais mstaafu Kikwete kuanzisha taasisi hiyo imeonesha uzalendo na utayari wake wa kuendelea kutoa mchango wake kwa nchi yake na Bara la Afrika kwa ujumla kwani taasisi hiyo itatoa huduma zake ndani na nje ya nchi yetu,"amesema.



AZUNGUMZIA VIPAUMBELE VYA TAASISI

Rais Dk.Magufuli ameeleza namna ambavyo amefurahishwa na vipaumbele vyake katika kuwatumikia Watanzania na Bara la Afrika kwa ujumla.Amefafanua kuna vipaumbele vinne na kipaumbele cha kwanza ni eneo la afya na Watanzania wanafahamu umuhimu wa eneo la afya kwani ili nchi iwe na maendeleo lazima watu wake wawe na afya njema.

Amesema Serikali yake imeendelea na jitihada za kuhakikisha inapunguza vifo kwa mama mjazito na watoto chini ya miaka mitano na kufafanua kuwa Rais mstaafu Kikwete akiwa madarakani alifanikiwa kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wenye umri chini ya miaka mitano.

"Nimefurahi kuona suala la afya limepewa kipaumbele kwenye taasisi hii mpya ambayo naizindua leo hii. Nami kwenye Serikali nimeendelea kuboresha vituo vya afya na sasa tunaendelea na upanuzi wa vituo vya afya 170 ambapo lengo viwe vinafanya upasuaji kwa mama wajawazito ili kuokoa
maisha,"amesema Rais Dk Magufuli na kuongeza wanaendelea na kutoa chanjo kwa watoto chini ya miaka mitano na lengo ni kupunguza vifo,"amesema.


Amesema kipaumbele cha pili ni vijana na kueleza kuwa  kuna changamoto nyingi katika kundi hilo ambalo linahitaji kusaidiwa na taasisi ya Rais mstaafu Kikwete imeamua kuelekeza nguvu zake wakati kipaumbele cha tatu ni sekta ya kilimo na kwa Tanzania sehemu kubwa ya watu wake wamejikita kwenye sekta hiyo.Kipaumbele cha nne ni utawala bora na amani na kufafanua nalo ni eneo muhimu na kueleza vipaumbele vyote hivyo navyo ndivyo vipaumbele vyake na hata kwa nchi nyingine za Afrika.

"Taasisi hii imeahidi kushirikiana na Serikali na si kushindana.Hivyo tutahakikisha tunashirikiana nayo kwa karibu na nieleze tu sitakuwa tayari kushirikiana na taasisi yenye lengo la kuvuruga amani ya nchi na ninakushukuru mzee Kikwete umeeleza wazi namna ambavyo utashirikiana nasi,"amesisitiza.

Rais Magufuli ameeleza namna ambavyo anamshukuru Rais mstaafu Kikwete na kufafanua hata yeye kuwa Rais imetokana na yeye na huo ndio ukweli, hivyo popote atakapomuana ataendelea kumshukuru. Pia amewashukuru viongozi wengine wa ngazi mbalimbali na anafurahia kuona wapo marais wastaafu wamemzunguka na kumpa ushauri na maelekezo yanayomsaidia kutekeleza majukumu yake.

KIKWETE AMSHUKURU DK MAGULI, AZUNGUMZIA TAASISI YAKE

Kwa upande wake Rais Mstaafu Kikwete amesema kuwa anamshukuru Rais Magufuli kwa kukubali kuzindua taasisi hiyo na kuipa heshima ya hali ya juu na kutumia nafasi hiyo kuahidi kuwa lengo la kuanzishwa kwa taasisi hiyo ni kufanya kazi katika maeneo ambayo wameamua kuanza nayo zaidi kama sehemu ya kutoa mchango wao katika kushirikiana na Serikali kutekeleza majukumu yake.

Amefafanua wakati anakaelekea kustaafu , alianza kufikiria akiwa na wasaidizi wake nini afanye baada ya kustaafu na hivyo walikubaliana mambo mawili, moja kuanzisha taasisi hiyo na mbili kuandika kitabu ambacho nacho atakifanikisha.

Amelezea maeneo ambayo wamekubaliana na bodi ya wadhamini wa taasisi hiyo ya kuanza nayo na kufafanua wanatambua yapo maeneo mengi lakini wameanza na mambo manne likiwemo eneo la afya ya mama mjazito na mtoto."Ni falsafa na sera ya msingi kuwa tutafanya kazi kwa karibu na Serikali na hakuna sababu ya kusigana na Serikali na hatutakubali kushawishiwa na mtu yoyote."

Ameongeza Serikali ndio washirika namba moja na kueleza kuwa hivyo wao wanachokifanya ni kuendelea kusaidia kazi inayofanywa na Rais Dk.Magufuli na nchi nyingine za Afrika.Shabaha yao ni kwamba pale ambao wengine wapo wao hawatakwenda na hata wakienda basi ni kuongeza nguvu na kubwa zaidi hakuna wanayeshindana naye.

"Nakushukuru Rais kwa moyo wako wa upendo kwangu na Watanzania kwa ujumla na kwamba kazi kubwa ya kuleta maendeleo ambayo unaifanya sote tunaiona.Natambua kunachangamoto nyingi ambazo unakabiliana nazo lakini tutaendelea kukuombea kwa Mungu ili utekeleze vema majukumu
yako,"amesema Rais mstaafu Kikwete.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: