Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Paul Makonda amewatahatharisha wakazi wa jijini hapa kuwa makini kwa siku ya kesho ambapo kutokana na utabili wa hali ya hewa inatarajiwa kuwa na mwendelezo wa mvua kubwa hivyo kuwataka kuwa makini wakati wote.

Makonda amesema hayo leo alipotembelea maeneo ya Vingunguti na kujionea athari zilizojitokeza ambapo nyumba zaidi ya 17 zimesombwa na maji kutokana na mto wa maji kuhama na kupita kwenye makazi ya watu na kusababisha kaya hizo kukosa makazi.

"Ninawaomba wananchi wangu wa Dar es salaam hususani waishio bondeni wahame pia waendesha vyombo vya moto wawe makini kipindi hiki cha mvua kubwa ambazo zinaendelea kunyesha na kesho kama huna sababu ya kutoka nyumbani basi ni vizuri usitoke kwani utabili unaonyesha kesho kutakuwa na mvua kubwa zaidi ya hii inayoendelea kunyesha" amesema Makonda.

Kwa upande wake naibu Meya wa Manispaa ya Ilala Omary Kumbilamoto amesema kuwa mto huo umehama na kwa sasa amewataka wananchi wote ambao wako jirani na eneo hilo kuhama ili kuepusha madhara zaidi ambayo yanaendelea kujitokeza ambapo nyumba zaidi ya 17 zimesombwa maji.

Aidha Kumbilamoto akimueleza Mkuu wa Mkoa jitihada mbalimbali ambazo wamekuwa wakizifanya amesema kuwa wananchi wenyewe wamechangia fedha ili kudhibiti madhara hayo ambapo kwasasa wamefanikisha kupata kiasi cha zaidi ya shilingi milioni mbili ili kuondoa taharuki inayoendelea kuongezeka.

"Mpaka sasa tumefanya jitihada tukishirikiana na wakazi wa eneo hili na tumechanga pesa zaidi ya milioni mbili kwa ajili ya kueresha njia halisi ya mto huu na tumewasiliana na manispaa ili kuja kutuonyesha mipaka na kwa sasa wao ndo wanachelewesha jitihada hizi"  amesema Kumbilamoto.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: