BEKI wa kati wa Yanga, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ amesema anawasubiri kwa hamu washambuliaji wa Simba, Emmanuel Okwi na John Bocco ili awaonyeshe kazi kuthibitisha ubora wake kwa sasa.

Simba inaongoza kwa pointi 55, nyuma ya Yanga wenye pointi 47 katika Ligi Kuu Bara na timu hizo zitakutana Aprili 29, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam katika mchezo wa ligi hiyo.

Beki huyo ambaye muda mrefu hakuwa akipata nafasi kikosini Yanga, hivi karibuni alicheza mechi ya kwanza ya kimataifa ya Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Wolaita Dicha ya Ethiopia.

Ninja pia katikati ya wiki hii alicheza mechi ya ligi kuu dhidi ya Singida United na kuifungia Yanga bao moja na kutoka sare ya bao 1-1.

Akizungumza na Championi Jumamosi, Ninja alisema; “Nimekuwa nikibezwa sana ila nafasi ya kucheza imeniongezea vitu na kunifanya nizidi kuwa bora japokuwa bado sijafikia katika kiwango changu.

“Nikipata nafasi ya kucheza dhidi ya Simba, nataka kuwaonyesha washambuliaji wao na zaidi mipira ya juu nitaicheza kwa ustadi mkubwa na naamini washambuliaji wao hawataleta madhara.”
Share To:

msumbanews

Post A Comment: