Mbunge wa Mtama, Nape Nnauye ameuliza serikali imefikia wapi kutafuta soko la Mbaazi baada ya msimu uliopita matatizo ya soko kushusha bei kutokaTshs 2,000 mpaka 150. Amesema serikali iliahidi Bungeni kuwa itahakikisha inahangaika kupata soko la kuaminika la zao hilo.

Nape amesema sasa ni msimu wa kilimo hicho, kama bado hali haieleweki wananchi washauriwe waachane na mbaazi na badala yake wajikite kwenye mazao mengine ambayo yana soko la uhakika.

Akijibu swali hilo naibu waziri wa kilimo, Eng. Stella Manyanya amemjibu kuwa ni kweli hakukuwa na hali inayoridhisha kwenye soko la mbaazi na ni kutokana na wadau waliokuwa wanategemewa sana ilikuwa ni India.

Eng. Stella amesema mbaazi ni chakula kizuri chenye protini na watanzania wanaweza kula badala ya kuwategemea watu wa maeneo mengine. 

Amesema biashara ni ushindani na kila watu wanahakikisha wanakidhi soko lao la ndani, upande wa Tanzania wanaendelea kutafuta soko lakini wakati huo huo wanaendelea kusisitiza watu wapende kutumia mbaazi.

Amesema Dodoma Mbaazi inauzwa mpaka 1,800 kwa kilo na soko la Dar es Salaam kwenye supermarket inauzwa mpaka 2,400 hivyo tusitegemee soko mpaka kutoka nje kwani hata ndani ya nchi bado kuna watu wanaweza kula mbaazi yeye akiwa mmojawapo pia inategemewa hata mashule yanaweza kutumia wakati masoko yanaendelea kutafutwa.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: