Wasanii maarufu wa muziki wa Bongo Fleva, Diamond Platnumz na Ali Kiba wamekutana katika msiba wa Agnes Masogange na kusalimiana.

Mara baada ya wasanii hao kusalimiana kwa kupeana mikono wakiwa katika meza kuu, waombolezaji waliojaa kwenye Viwanja vya Leaders walipiga kelele.

Diamond alimsalimia Kiba kwa kumpa mkono, kisha wawili hao walikumbatiana na baada ya tukio hilo, MC Pilipili alisikika akisema: “Unaona sasa, hawana ugomvi hawa.”

Kumekuwa na taarifa za wanamuziki hao kuwa na ugomvi kwa muda mrefu ambao hata hivyo, unatajwa kutengenezwa na mashabiki wao wa ‘Team Kiba na Team Diamond.’

Akizungumzia katika viwanja hivyo, Ali Kiba ambaye ametoka kuchukua jiko hivi karibuni, amesema harusi na kifo vyote ni ibada na ndiyo maana amefika kuungana na waombolezaji wengine ingawa bado yupo fungate.

Masogange alifariki dunia juzi katika Hospitali ya Mama Ngoma, Mwenge ambako alilazwa kwa siku nne.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: