Kiungo wa Simba, Jonas Mkude (katikati) akiongea jambo.
KIUNGO wa Simba, Jonas Mkude gari limewaka kwani amesema kwa sasa yupo fiti kucheza baada ya kuanza mazoezi ya pamoja na kikosi cha timu hiyo akiwa ametoka katika majeraha aliyoyapata hivi karibuni.

Mkude alipatwa na majeraha ya mguuni hivi karibuni akiwa mazoezini baada ya kugongana na Mzamiru Yassin wakijiandaa na mchezo dhidi ya Njombe Mji kwenye Uwanja wa Boko Veteran jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na Mwandishi wetu Mkude alisema kuwa, kwa sasa anaendelea vizuri na mazoezi na yupo fiti kucheza iwapo Kocha Pierre Lechantre ataamua kumpa nafasi kikosini.

Alisema tatizo lake limeisha na ameshaanza mazoezi ya pamoja na wenzake kwa siku ya nne sasa na kudai kuwa yupo tayari kucheza mchezo wa ushindani.

“Kwa sasa naendelea vizuri na nipo fiti, nimeshaanza mazoezi ya pamoja na wenzangu kwa siku nne na sijapata tatizo lolote lile.

“Kocha ndiye atakayeamua juu ya kunichezesha ama kutonichezesha katika mchezo ujao kwa kuwa nimetoka kwenye majeraha lakini afya yangu ipo vizuri,” alisema Mkude. Simba keshokutwa Jumatatu itacheza na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro katika mwendelezo wa Ligi Kuu Bara.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: