Serikali imesema kanuni mpya za maudhui kwenye mitandao, runinga na redio zimetungwa kwa lengo la kudhibiti usambazaji wa kauli chafu, matusi, picha za utupu na zenye maudhui yasiyofaa kwa watoto.

Kanuni hizo zimetungwa ikiwa ni utekelezaji wa Sheria ya Mawasiliano ya Kiektroniki na Posta ya Mwaka 2010.

Pia imesema itaendelea kuhamasisha utengenezaji na uzalishaji wa maudhui ya ndani yanayozingatia maadili, mila na desturi za Mtanzania huku ikikiri kuwapo kwa mmomonyoko wa maadili kunakoongezeka siku hadi siku, hivyo imejipanga kukabiliana na changamoto hiyo.

Akiwasilisha bungeni mjini hapa jana hotuba ya makadirio ya bajeti ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Waziri wa wizara hiyo, Dk. Harrison Mwakyembe, alisema kanuni hizo zinamtaka kila mtumiaji wa mitandao awe na namba ya siri ili 'wajanja' wasitumie kirahisi chombo chake cha mawasiliano kutenda matendo yanayokwenda kinyume cha sheria.

Alisema kanuni hizo pia zinaweka muda maalumu kwa picha mgando na nyongevu za filamu au muziki wenye maneno yasiyofaa kwa watoto kuonyeshwa kwenye runinga.

"Tuliweka muda huo maalumu kuanzia saa 4:00 usiku hadi saa 11:30 asubuhi, lakini wadau wamekuwa wakali, wanadai picha na nyimbo hizo zirushwe kuanzia saa 6:00 usiku wakati watoto wamelala na mwisho saa 11:00 asubuhi, kabla watoto hawajaamka," alisema Dk. Mwakyembe.

Aliongeza kuwa kanuni hizo zinataka madaraja yawekwe kwa kila filamu, video, wimbo au albamu kutoka ndani au nje ya nchi ndipo kazi hizo zitumike kwenye vyombo vya utangazaji.

"Msingi wa kanuni hizi ni kuhakikisha teknolojia inatutumikia badala ya kututumikisha na kuvuruga mustakabali wa maadili ya taifa letu. Ni kanuni zilizozingatia mazingira yetu halisi kama kila Watanzania," alisema.

Dk. Mwakyembe alisema, mmomonyoko wa maadili ya Kitanzania unaoongezeka siku hadi siku, ni miongoni mwa changamoto zinazoikabili wizara yake.

Alisema wanaendelea kutoa elimu kupitia vyombo vya habari na kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kuzingatia maadili, mila na desturi za Kitanzania.

Ili kutekeleza majukumu yake kwa mwaka ujao wa fedha, Dk. Mwakyembe aliliomba Bunge kuidhinisha bajeti ya Sh. bilioni 33.3. Kati yake, Sh. bilioni 12.2 ni mishahara, Sh. bilioni 9.3 kwa ajili ya matumizi mengine na Sh. bilioni 8.7 za utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: