Na: Lilian Lundo – MAELEZO, Dodoma.
Kamati za maafa za Mikoa na Wilaya kufanya tathimini ya kujua miundombinu iliyoharibiwa na mvua zinazoendelea kunyesha hapa nchini  ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameyasema hayo leo Bungeni, Mjini Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mhe. Hussein Nassor juu ya mpango wa serikali  kurejesha miundombinu iliyoharibiwa na mvua zinazoendelea nchini.

“Kipindi hiki tumeendelea kupata mvua nyingi nchini, ambazo zimesababisha maafa, Nawapa pole wale waliopoteza ndugu zao na kuharibiwa na miundombinu kutokana na mvua hizo,” alisema Waziri Mkuu.

Amesema, Serikali inaendelea kujipanga kuhakikisha miundombinu yote iliyoharibiwa na mvua zinazoendelea inarejeshwa katika hali yake kupitia kamati za maafa za mikoa na wilaya kwa kushirikiana na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) pamoja na Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA).

Hata hivyo, amewataka wakulima kutumia mvua zinazoendelea kunyesha kwa kulima mazao ya chakula na biashara kwani Serikali imejipanga vyema kushirikiana na wakulima kutafuta masoko ya mazao hayo ndani na nje ya nchi.

Aidha Waziri Mkuu, ametoa wito kwa wananchi wanaoishi mabondeni kuhama kwani mvua zinazoendelea kunyesha zinaweza kuleta madhara  makubwa zaidi ikiwa ni pamoja na kupoteza maisha.

Vile vile Mhe. Majaliwa amesema, Serikali  imetoa shilingi Bilioni 160 kwa ajili ya kujenga na kuimarisha vituo vya afya ngazi za wilaya nchi nzima ikiwa ni sehemu ya mikakati ya Serikali kuimarisha huduma za afya hapa nchini.

Ameendelea kwa kusema, lengo la Serikali ni kuhakikisha vituo hivyo vya afya vinakuwa na chumba cha maabara, chumba cha upasuaji pamoja na chumba kwa ajili ya huduma ya mama na mtoto.

Amesema, ujenzi huo wa vituo vya afya unaenda sambamba na ujenzi wa nyumba ya mganga mkuu katika kila kituo.

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limeweka utaratibu wa wabunge wa bunge hilo kumuuliza maswali ya papo kwa papo Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa kila siku ya Alhamisi katika mikutano yote ya Bunge
Share To:

msumbanews

Post A Comment: