Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameitaja mikoa ya Tabora, Geita, Mtwara na Shinyanga kuwa inaongoza kwa utoro wa wanafunzi wa sekondari.

Waziri mkuu pia ameitaja mikoa ya Rukwa, Geita, Tabora, Singida na Simiyu kuwa inaongoza kwa utoro wa wanafunzi wa shule za msingi.

Majaliwa ambaye pia ni mbunge wa Ruangwa ameitaja mikoa hiyo leo Jumatatu Aprili 2,2018 akizindua mbio za Mwenge wa Uhuru katika uwanja wa Magogo mkoani Geita.

Mbio za Mwenge zitakazohitimishwa Oktoba 14,2018 mkoani Tanga zinaongozwa na kauli mbiu “Elimu ni ufunguo wa maisha, wekeza sasa kwa maendeleo ya nchi yetu.”

Majaliwa amesema Mkoa wa Tabora unaongoza kwa asilimia 9.7 ya wanafunzi watoro wa sekondari ukifuatiwa na Geita (asilimia 8.1), Mtwara (asilimia 6.1) na Shinyanga (asilimia 6.3).

Kwa shule za msingi, Rukwa inaongoza kwa asilimia 3.2, ukifuata Geita (asilimia 3.1), Tabora (asilimia 2.9), Singida (asilimia 2) na Simiyu (asilimia 2).

“Kwa jumla utoro wa wanafunzi wa sekondari ni mkubwa kuliko shule za msingi. Naikumbusha mikoa yote niliyoitaja kuhamasisha wananchi wakiwamo wazazi na walezi kuhusu umuhimu wa elimu na mahudhurio endelevu shuleni kwa kutumia utaratibu wa sheria zilizowekwa,” amesema Majaliwa.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: