Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, linamshikilia Mbunge wa Tarime Vijini, John Heche (Chadema), kwa tuhuma za kushindwa kuripoti polisi kama alivyotakiwa na jeshi hilo.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amethibitishwa kushikiliwa kwa mbunge huyo tangu jana.

Mambosasa amesema Heche alikamatwa kwa kosa sawa na lile lililokuwa likimkabili Mbunge wa Kawe, Halima Mdee, ambaye pia alishindwa kuripoti polisi wiki iliyopita baada ya kwenda Afrika Kusini kwa matibabu kabla ya kukamatwa Uwanja wa Ndega wa Dar es Salaam (JNIA), usiku wa kuamkia juzi.

Aidha, Mambosasa amesema endapo taratibu zitakamilika mbunge huyo anaweza kufikishwa mahakamani leo, kuunganishwa katika kesi ya viongozi wengine wa chama hicho waliopata dhamana jana.

“Ni kama alivyoshikiliwa mwenzake Mdee naye hakuripoti, walikuja wakatakiwa kurudi wote wao hawakurudi, hakuna kosa jipya kosa lake ni kutorudi hadi wenzake wanapelekwa mahakamani,” amesema Mambosasa.

Machi 27 mwaka huu Heche alishindwa kuripoti polisi pamoja na viongozi wengine saba wa chama hicho kama walivyotakiwa na jeshi hilo akidai alikuwa na msiba.

Viongozi hao ni Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Katibu Mkuu wa chama hicho, Vincent Mashinji, Naibu Katibu Mkuu Bara, John Mnyika, Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Salum Mwalimu, Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa na Mbunge wa Tarime Mjini, Esther Matiko ambao wanakabiliwa na mashtaka manane yakiwamo kuhamasisha maandamano, uchochezi na uasi.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: