Mzee John Mkubila
akizungumza juu ya suala la kumuoa Binti wa miaka kumi na tatu wakati
alipokuwa amekamatwa na jeshi la polisi jamii.
***
Jeshi la Polisi Mkoani Geita
linamshikilia mzee wa miaka sitini na tisa (69) kwa kosa la kumuoa
binti mwenye umri wa miaka 13 ambaye mkazi wa kitongoji cha Rwenge
kijiji cha Bugalama.
Mzee John Mkubila ambaye ni mkazi wa
mtaa wa mwembeni kata ya Nyankumbu mjini Geita amekiri kumuoa binti huyo
kwa makubaliano ya mzazi wa binti huyo kuwa awe anamsaidia kazi za
nyumbani kutokana na mke wake kuwa na majukumu mengi ya kibiashara hali
ambayo imepelekea kujikuta mzee akikosa huduma za msingi na kuamua
kumuoa binti huyo.
“Nilionana na baba yake nikamwambia
kuwa kwa sasa umri wangu umekwenda naweza kupata binti mdogo wa
kunisaidia maana kwangu nina mke ila ana majukumu mengi hivyo najikuta
nashindwa kufanya shughuli zingine baba yake akaniambia sawa ndio akawa
amenipa huyu ambaye kwa sasa ni Mke Mdogo”,alisema Mzee Mkubila.
Aidha binti huyo amekiri kuolewa kutokana na na baba yake mzazi kumlazimisha.
“Mimi nilikataa kuolewa lakini baba
yangu ndiye alinilazimisha niolewe kutokana na kwamba nimemaliza shule
ya msingi ila mimi sikuwa tayari kuolewa kutokana na umri wangu kuwa
mdogo”,alisema binti huyo.
Hata hivyo kwa baadhi ya wananchi ambao
walikuwa wamejitokeza kwenye ofisi za polisi jamii kwenye mtaa huo
wamesikitishwa na kitendo hicho na kuitaka jamii kubadilika na kuachana
na desturi ambazo zimeendelea kuwakandamiza watoto wa kike.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Geita Mponjoli
Mwabulambo amesema nyuma ya tukio kulikuwa na mapatano baina ya wazazi
wa mtoto na huyo mzee kama mahari ilitolewa lakini pia uchunguzi
unafanyika na utakapokamilika wote watafikishwa mahakamani kwa kuwa ni
kosa la kisheria kujamiana na mtoto mwenye umri wa chini ya miaka kumi
na tano(15).
Chanzo- Madukaonline
Post A Comment: