Mzee John Mkubila akizungumza juu ya suala la kumuoa Binti wa miaka kumi na tatu wakati alipokuwa amekamatwa na jeshi la polisi jamii.
***
Jeshi la Polisi Mkoani Geita linamshikilia mzee  wa miaka sitini na tisa (69) kwa kosa la kumuoa binti mwenye umri wa miaka 13 ambaye mkazi wa kitongoji cha Rwenge kijiji cha Bugalama.


Mzee John Mkubila ambaye ni mkazi wa mtaa wa mwembeni kata ya Nyankumbu mjini Geita amekiri kumuoa binti huyo kwa makubaliano ya mzazi wa binti huyo kuwa awe anamsaidia kazi za nyumbani kutokana na mke wake kuwa na majukumu mengi ya kibiashara hali ambayo imepelekea kujikuta mzee akikosa huduma za msingi na kuamua kumuoa binti huyo.

“Nilionana na baba yake nikamwambia kuwa kwa sasa umri wangu umekwenda naweza kupata binti mdogo wa kunisaidia maana kwangu nina mke ila ana majukumu mengi hivyo najikuta nashindwa kufanya shughuli zingine baba yake akaniambia sawa ndio akawa amenipa huyu ambaye kwa sasa ni Mke Mdogo”,alisema Mzee Mkubila.

Aidha binti huyo amekiri kuolewa kutokana na na baba yake mzazi kumlazimisha.

“Mimi nilikataa kuolewa lakini baba yangu ndiye  alinilazimisha niolewe kutokana na kwamba nimemaliza shule ya msingi ila mimi sikuwa tayari kuolewa kutokana na umri wangu kuwa mdogo”,alisema binti huyo.

Hata hivyo kwa baadhi ya wananchi ambao walikuwa wamejitokeza kwenye ofisi za polisi jamii kwenye mtaa huo wamesikitishwa na kitendo hicho na kuitaka jamii kubadilika na kuachana na desturi ambazo zimeendelea kuwakandamiza watoto wa kike.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Geita Mponjoli Mwabulambo amesema nyuma ya tukio kulikuwa na mapatano baina ya wazazi wa mtoto na huyo mzee kama mahari ilitolewa lakini pia uchunguzi unafanyika na utakapokamilika wote watafikishwa mahakamani kwa kuwa ni kosa la kisheria kujamiana na mtoto mwenye umri wa chini ya miaka kumi na tano(15). 

Chanzo- Madukaonline
Share To:

msumbanews

Post A Comment: