Jumuiya ya Taasisi za Vyuo vya Elimu ya Juu Tanzania (TAHLISO) imewataka wanafunzi wote wa vyuo vikuu nchini kuwa watulivu wakati serikali ikiendelea na uchunguzi wa kifo cha Akwilina Akwilin aliyeuawa kwa kupigwa risasi Februari 16, mwaka huu.

Wito huo umetolewa leo na Mwenyekiti wa Seneti ya TAHLISO, George Mnali wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma kuhusiana na msimamo wa Jumuiya hiyo kuhusu kifo cha mwanafunzi mwenzao huyo.
Mnali amesema kuwa wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu nchini wanapaswa kuwa watulivu na wavumilivu wakati vyombo vya usalama vikiendelea na uchunguzi wake kuhusiana na kifo hicho kama ambavyo wameendela kuwa watulivu.
Mbali na hilo amevitaka vikundi mbalimbali ambavyo vimejitokeza kuwasemea wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu kuacha mara moja tabia hiyo kwa kuwa chombo pekee cha kuwasemea wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu ni TAHLISO peke yake.
Ameongeza kuwa wamegundua vikundi hivyo vinatumika kisiasa na vina lengo la kuharibu amani ya nchi kwa kuwa vinawataka baadhi ya viongozi kujiuzulu na wakati hata matokeo ya uchunguzi wa tukio hilo bado haujatoka.
Pia amewatupia lawama wanasiasa kwa kushindwa kulinda kauli zao ambazo ndizo zilikuwa chanzo cha tukio hilo.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: