Serikali imekanusha taarifa zilizotolewa na baadhi ya vyombo vya habari kwamba, imekizuia Kiwanda cha Sukari Zanzibar, ZSFL, kuuza Sukari yake Tanzania Bara.
Akizungumza na wandishi wa habari leo jijini Arusha, Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali, Dk. Hassan Abbas, amefafanua kwamba, kiwanda hicho kinapaswa kukidhi soko la Zanzibar la tani elfu 10 badala ya kulalamika kimezuiwa kuuza Sukari nje.
 Dk. Abbas amesema, mahitaji ya kawaida Zanzibar ya sukari ni Tani 17,000 hadi 20,000 kwa mwaka, lakini kiwanda hicho, kina uwezo wa kuzalisha tani elfu 10 japo kwa sasa uzalishaji umeshuka hadi tani elfu 8 hivyo kufanya Zanzibar kuwa na upungufu wa tani elfu 9 hadi elfu 12.
 Mapema wiki hii Kaimu Mkurugenzi Mkuu Kiwanda hicho cha Sukari Zanzibar, Bi. Fatma Salum Ali, alisema kiwanda hicho kinapata hasara ya shilingi 387,000 kwa kila tani moja ya Sukari inayozalishwa kutokana na kushindwa kupata kibali cha kuuza Sukari Tanzania Bara ambako kuna soko shindani kwa misingi ya gharama za uzalishaji na bei.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: