Chipukizi wa klabu ya Manchester United Marcos Rashford leo ameibuka mchezaji bora wa mechi ya ligi kuu nchini England dhidi ya Liverpool baada ya kufunga mabao mawili yaliyoipa ushindi timu yake.
Mchezo huo ambao umemalizika jioni hii kwenye uwanja wa Old Trafford, ulikuwa wa vita ya kuwania nafasi ya pili baada ya mbio za ubingwa kutawaliwa na Manchester City.
Ilimchukua dakika 14 kinda huyo mwenye umri wa miaka 20 kuifungia bao la kuongoza timu yake baada ya kutumia mpira wa 'Counter Attack' na kuwahadaa walinzi wa Liverpool kabla ya kuachia mkwaju mkali uliozama nyavuni.
Baada ya bao la kwanza ilimchukua dakika 10 na sekunde kadhaa kufunga bao la pili akitumia vizuri makosa ya walinzi wa Liverpool baada ya kaqzi nzuri iliyofanywa na Lukaku.
Liverpool walifanikiwa kupata bao moja dakika ya 66 baada ya mshambuliaji Sadio Mane kupiga mpira uliombabatiza mlinzi Eric Bailly aliyerejea kutoka majeruhi na kujifunga hivyo mechi kumalizika United kushinda 2-1.
Kwa matokeo hayo sasa huenda Man United ikawa imejiweka kwenye mazingira mazuri ya kumaliza katika nafasi ya pili ambapo imefikisha alama 66 mbele ya Liverpool yenye alama 60 na nyuma ya Man City yenye alama 78.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: