Rais wa Tanzania Dkt. Magufuli leo amemsihi  Waziri wa Ulinzi wa Israel Mhe. Avigdor Lieberman kumfikishia ujumbe Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu  kwamba anamualika nchini Tanzania pamoja na kumuomba kufungua ubalozi nchini.
Rais Magufuli ametoa ombi hilo kwa waziri wa Israel ammbapo amemfahamisha kwa sasa ubalozi unaotumika ni ule uliopo Nairobi nchini Kenya.
Aidha Mhe. Rais ametaka makubaliano ya ushirikiano kati ya Tanzania na Israel katika maeneo mbalimbali yakiwemo ulinzi na usalama, mafunzo na masuala ya kiuchumi yatiwe saini haraka ili utekelezaji uanze mara moja.
Pamoja na hayo Rais amemshukuru Mhe. Lieberman kwa kuitembelea Tanzania na amemhakikishia kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ina dhamira ya dhati ya kuukuza zaidi na kuuimarisha uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na Israel.
Mazungumzo hayo yamehudhuriwa na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Balozi wa Israel hapa nchini Mhe. Noah Gal Gendler, viongozi wakuu wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) na Jeshi la Polisi.
Kwa upande wake Mhe. Avigdor Lieberman amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kumkaribisha na kufanya nae mazungumzo na pia amemhakikishia kuwa Israel imejipanga kuongeza uhusiano na ushirikiano wake na Tanzania katika maeneo yote ya makubaliano pamoja na kusaidia kilimo na usindikaji wa chakula.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: