MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuhukumu mfanyabiashara Stanley Mwaura kutumikia kifungo cha miaka miaka 2827 jela baada ya kupatikana na hatia ya makosa 419 ikiwemo utakatishaji  fedha.

Hukumu hiyo imetolewa leo na Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi baada ya kumaliza kusikiliza ushahidi wa upande wa mashtaka na utetezi.

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Shaidi amesema upande wa mashtaka kupitia mashahidi wake  15 waliofika mahakamani hapo kutoa ushahidi, wamethibitisha mashtaka pasipo kuacha shaka kuwa mshtakiwa alitenda makosa hayo.

Katika kesi hiyo mshtakiwa alijitetea mwenyewe.

Hakimu Shaidi amesema,  mshtakiwa huyo ana makosa 419, ambapo kosa la 1 hadi 99 ni kughushi, kosa la 100 hadi 198 ni kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu, kosa la 199 hadi 297 kujipatia nyaraka kwa njia ya uongo.  Huku kosa la 298 hadi 396 ni utakatishaji fedha na kosa la 397 hadi 419 ni kughushi.

Hakimu Shaidi amesema kuwa katika kosa la 1 hadi 99 Mahakama inamuhukumu mshtakiwa Murithi kwenda jela miaka 7 kwa kila kosa.

Katika kosa la 100 hadi 198 la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu Mahakama inamuhukumu kwenda jela miaka 7 kwa kila kosa.

Pia kosa la 199 hadi 297 mshtakiwa anahukumiwa kwenda jela miaka 7 kwa kila kosa.

Katika kosa la 298 hadi 396 mshtakiwa amehukumiwa kulipa faini ya Sh. milioni 100 kwa kila kosa sawa na Sh.bilioni 9.9 ama kutumikia kifungo cha miaka miaka 6 gerezani kwa kila kosa.

Pia kosa la 397 hadi 419 amehukumiwa kwenda jela miaka 7 kwa kila kosa.

"Mahakama imekutia hatiani katika makosa hayo 419 ambapo unahukumiwa kwenda jela miaka 7 kwa kila kosa ambapo jumla itakuwa miaka 2827 lakini adhabu hii itaenda sambamba ambapo utatumikia miaka 7 tu gerezani," amesema Hakimu Shaidi.

Miongoni mwa mashtaka yaliyokuwa yakimkabili mshtakiwa ni utakatishaji fedha ambapo inadaiwa kati ya February 6 na 7,mwaka 2012 maeneo ya Jiji la Dar es Salaam alijihusisha katika muamala wa kuhamisha fedha ambazo ni Sh.Mil 4.9 kinyume na sheria.

Pia inadaiwa kati ya April 30 na Mai 5, mwaka 2013 alihamisha kiasi cha Sh.milioni 6.5 kinyume na sheria
Share To:

msumbanews

Post A Comment: