Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimesema Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda wamekiuka sheria na Katiba ya nchi kwa kauli zao zinazoashiria kumhukumu Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP), Abdul Nondo.

Nondo ambaye ni mwanafunzi wa mwaka wa tatu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), alidaiwa kutoweka usiku wa kuamkia Machi 6, 2018 na kupatikana usiku wa Machi 7 huko Mafinga, Iringa na kujisalimisha polisi.

Taarifa ya kituo hicho iliyotolewa jana Alhamisi Machi 15, 2018 na mkurugenzi mtendaji wake, Hellen Kijo-Bisimba imesema kutokana na kauli za viongozi hao pamoja na za Jeshi la Polisi, wameamua kutoa ufafanuzi wa kisheria

 “Dhana ya kutokuwa na hatia kwa mujibu wa Ibara ya 13 (6) (b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, Sura namba mbili kama ilivyofanyiwa marejeo mwaka 2002. Ni marufuku kwa mtu yeyote aliyeshtakiwa kwa kosa la jinai kutendewa kama mtu mwenye kosa hilo mpaka itakapothibitika kuwa anayo hatia ya kutenda kosa hilo,” amesema.

Amesema ni kosa kumhukumu mtu yeyote bila ya chombo chenye mamlaka hayo kuthibitisha kuwa mtu huyo amefanya kosa hilo.
Amesema kutokana na hilo viongozi wa kisiasa na Serikali kuzungumza baadhi ya masuala kama maamuzi ya mwisho na kuingilia mhimili wa mahakama na kuwaita watu wahalifu na kusahau dhana pana  ya kutokuwa na hatia hadi imethibitishwa, ni ukiukwaji wa Katiba.

Amebainisha kuwa wanapaswa kuelewa kwamba Mahakama ndio chombo chenye mamlaka ya juu zaidi katika utoaji haki kama ilivyofafanuliwa katika Ibara ya 107A (1) ya Katiba.
Amesema viongozi wa Serikali na polisi watafanya kosa kumshutumu mtu yeyote yule na kuingilia uhuru na kazi ya mhimili wa mahakama kinyume cha Katiba walioapa kuilinda.

Kuhusu haki ya kupata dhamana, mkurugenzi huyo amesema Katiba imetoa haki ya mtu kupata dhamana pale ambapo suala lake lipo katika vyombo vya utaoji wa haki.
 “Wakati haki na wajibu wa mtu yeyote inapohitajika kufanyiwa maamuzi na mahakama au chombo kingine chochote kinachohusika, basi mtu huyo atakuwa na haki ya kupewa fursa ya kusikilizwa kiukamilifu, na pia haki ya kukata rufani au kupata nafuu nyingine,” amefafanua.





Share To:

msumbanews

Post A Comment: