Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesema hakielewi lengo la Jeshi la Polisi mpaka sasa limekusudia kuwafanyia kitu gani viongozi wa Chadema kwa madai wanaitwa kila uchao halafu hakuna kinachojadiliwa kuhusiana na wito wao.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa Itifaki na Mawasiliano ya Mambo ya Nje wa Chadema, John Mrema amesema Mwenyekiti wa chama hicho Freeman Mbowe na Naibu Katibu Mkuu (Zanzibar), Salum Mwalimu walifika kituo cha Polisi Jijini Dar es Salaam kama walivyotakiwa hapo awali kufanya hivyo na mwishowe kuachiwa kurudi walipotoka bila ya kuhojiwa jambo lolote lile tangu walipofika hapo majira ya asubuhi.

"Ni kweli Mwenyekiti Freeman Mbowe na Naibu Katibu Mkuu (Zanzibar), Salum Mwalim waliripoti Polisi lakini hakukuwa na majadiliano ya aina yeyote yaliweza kufanywa siku ya leo.

Hatujui mpaka sasa Jeshi la Polisi linatutakia nini, kwa maana ninavyojua watu wakisha chukuliwa maelezo huwa Polisi wanaangalia kama watakuwa na kesi ya kujibu au laa, na kama itakuwepo basi wanapelekwa Mahakamani na kama hakuna basi jalada linafungwa. Sasa kwa upande wetu Jeshi la Polisi halijafunga jalada wanasema bado uchunguzi unaendelea", amesema Mrema.

Pamoja na hayo, John Mrema ameendelea kwa kusema "kwa kweli sisi mpaka sasa hivi tunaona ni usumbufu na hii sio mara ya kwanza maaana hata Edward Lowassa aliwahi kuitwa polisi akawa anahudhuria kila siku na mwisho wa siku hata hatujui lile jalada lilipotelea wapi walilokuwa wamempa juu ya kutoa kauli za uchochezi kwenye suala la Masheikh.

Sasa tunaona suala hili linajirudia kwa viongozi wetu wanaitwa kila siku, hawapelekwi mahakamani, jalada halifungwi huku ni kuwafanyia watu usumbufu kwa maana wengine ni wabunge kama Mbowe ametoka Mkoani Dodoma ambapo walikuwa wanajadili mpango wa bajeti anaitwa kuja kuripoti Polisi, sasa sijui gharama zote hizo nani atazilipa". aliendelea kusema Mrema

Kwa upande mwingine, viongozi wa Chadema wametakiwa kuripoti tena Polisi siku ya Alhamis (Machi 22, 2018) ambapo bado mpaka sasa haijafahamika wanachoitiwa tena.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: