Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amewataka wakala wa majengo nchini TBA kulipa madeni wanayodaiwa na Wananchi mbalimbali kufuatia ujenzi unaoendelea wa Shule ya Sekondari wavulana Ihungo iliyopo Wilayani bukoba mkoani kagera.

Waziri Ndalichako amesema kuwa tayari wizara imekwisha ilipa TBA  zaidi ya bilioni Tisa na garama ya ujenzi kwa mradi wote ni shilingi  bilioni 10 nukta 48.

" Mnyonge mnyongeni haki yake mpeni,  nipende kuwapongeza Wakala wa Majengo TBA kwa kazi nzuri ambayo wameifanya.

"Lakini nasikikitika sana kupokea malalamiko kutoka ofisi ya Mkuu wa mkoa inayoeleza kuwa bado kuna Wananchi wanaidai TBA kutokana na kutoa vifaa mbalimbali vya ujenzi kama vile mbao, matofali, na vibarua ambao wameshiriki katika ujenzi huo wa shule ya wavulana Ihungo na kuwa mpaka sasa hawajalipwa, hii haipendezi ni vyema TBA kuhakikisha inalipa madeni hayo,"alisema Waziri Ndalichako.

Waziri Ndalichako amesema haoni sababu kwa nini wananchi hawajalipwa wakati tayari Serikali imekwisha ilipa TBA, ni vyema wakalipwa ili kusaidia kuepusha migogiro isiyo ya lazima baina ya Serikali na wananchi.

Kwa upande wake Meneja wa TBA mkoa wa  Kagera Salum Chanzi amekiri kuwepo kwa sababu mbalimbali zilipelekea mradi kutokamilika kwa wakati na hivyo kuomba wapewe muda zaidi mpaka mwezi machi mwaka huu ili waweze kukamilisha.

"Mheshimiwa Waziri mradi huu haijakamilika kwa wakati uliokuwa umepangwa kutokana na changamoto ya kuagiza vifaa kutoka nje ya mji wa bukoba, na hii inatokana na bei wakati mwingine kuwa kubwa hapa bukoka  lakini nje ya hapa tunavipata kwa bro nafuu," alisema Chanzi.

Chanzi amemhakikishia Waziri Ndalichako kuwa tayari madeni yote wanayodaiwa na wananchi katika ujenzi huo wa Ihungo Sekondari yamewasilishwa katika ofisi yake na wahusika wote watalipwa.

Imetolewa na;
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini;
WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA.
15/2/2018


Share To:

msumbanews

Post A Comment: