Waziri Mkuu Mstaafu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani, Frederick Sumaye amefunguka na kuiomba serikali pamoja na vyombo vyake iwe inachukua hatua za haraka pindi yanapotokea matukio ya kiharifu yanayosababisha kupoteza uhai wa mtu.

Sumaye ametoa ombi hilo kwa serikali wakati alipokuwa amemaliza kutoa salamu za mwisho za marehemu Daniel John ambae aliyekuwa Katibu wa kata ya Hananasif katika Jimbo la Kinondoni ambapo mwili wake ulisaliwa kwenye Kanisa la Parokia ya Mtakatifu Anna Hananasif Kinondoni Jijini Dar es Salaam.

"Nimesikitishwa sana na kifo cha Daniel, alikuwa kiongozi wetu anafanya kazi za chama wala hakuwa na ugomvi na mtu. Tutaendelea kushirikiana na familia yake mpaka pale tutakapo mpumzisha", amesema Sumaye.

Pamoja na hayo, Sumaye ameendelea kwa kuongea "kwa niaba ya wapenda amani na haki naweza kusema Daniel hakufa kwa sababu ya CHADEMA bali amekufa kutokana na kupigania haki. Alitamani haki itendeke katika taifa hili. Naiomba serikali pamoja na vyombo vyake iwe inachukua hatua kuhakikisha mambo kama haya hayatokei na pale yanapotokea basi wachukue hatua za haraka kuhakikisha wahusika wanapelekwa katika vyombo vya sheria".

Kwa upande mwingine, Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limewaachia kwa dhamana viongozi waandamizi wa chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) walioitikia wito uliotolewa na jeshi la polisi siku ya jana (Jumatatu) na kutakiwa kurudi kituoni tena siku ya Jumanne wiki ijayo majira ya saa 4:00 asubuhi.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: