Mwanasheria Mkuu wa Kenya, Profesa Githu Muigai amejiuzulu nafasi hiyo aliyoitumikia kwa zaidi ya miaka sita. Na tayari Rais Uhuru Kenyatta amemteua Jaji Paul Kihara Kariuki kushika wadhifa huo.

Kwa upande wake, Rais Uhuru Kenyatta amemshukuru Profesa Githu kwa namna alivyolitumikia Taifa kwa weledi katika nafasi yake ya mwanasheria mkuu wa Serikali.

Profesa Muigai alitangaza leo kujiuzulu wadhifa huo alioteuliwa Agosti 27, 2011.

"Nimepokea kwa masikitiko uamuzi wa mwanasheria mkuu Githu Muigai. Namshukuru kwa huduma yake katika kipindi cha miaka sita na nusu. Nimemteua Jaji Paul Kiharara Kariuki,” Rais Uhuru Kenyatta alichapisha katika mtandao wake wa Twitter.

Profesa Muigai atakumbukwa kwa namna alivyokuwa mstari wa mbele kuwatetea watuhumiwa dhidi ya uhalifu wa binadamu uliotokana na vurugu za baada ya uchaguzi wa 2007 na kuendelea hadi 2008.

Vurugu hizo zilifunguliwa kesi kwenye Mahakama ya Jinai ya Kimataifa (ICC) iliyopo The Hague nchini Uholanzi na aliyekuwa mwendesha mashtaka mkuu, Luis Moreno-Ocampo.

Orodha ya watuhumiwa hao iliyofahamika kama ‘Ocampo six’ ni Rais Uhuru Kenyatta, Naibu wake William Ruto wakati huo alikuwa waziri wa Elimu, mawaziri wengine wa zamani Henry Kosgey, Francis Kirimi Muthaura, aliyekuwa mkuu wa polisi Mohammed Hussein Ali na mwandishi wa habari Joshua Arap Sang.

Pia, Profesa Muigai aliwahi kunukuliwa na vyombo vya habari vya Kenya akimtaka Mwendesha Mashtaka Mkuu wa ICC, Fatou Bensouda kuliheshimu Taifa la Kenya kwa kuonyesha weledi wakati wa kuendesha kesi iliyomkabili Rais Uhuru na wenzake, kwamba Kenya siyo Taifa lililoshindwa kutekeleza wajibu wake.

Hata hivyo, Profesa Muigai mwaka 2016 alipata changamoto baada ya muungano wa makanisa ya Kipentekoste kumtaka kujiuzulu kwa madai ya kushindwa kuishauri Serikali kuhusu masuala ya kidini.

Muungano wa makanisa hayo ulitoa hoja hiyo kufuatia kusajiliwa kwa kikundi cha watu waliokuwa wakidai hawamuamini Mungu, kwa madai anakwenda kinyume na katiba inayotambua uwapo wa Mungu
Share To:

msumbanews

Post A Comment: