Madiwani wa chama cha demokrasia na maendeleo (CHADEMA) wa halmashauri ya Arusha wameitaka halmashauri hiyo kufuta posho wanazopewa madiwani baada  ya mabaraza kufanyika kutokana na mgogoro uliojitokeza Februari 8 mwaka huu katika baraza lililopita.

Madiwani hao wamesema hayo Leo katika kikao cha kujadili rasimu ya mpango na bajeti kwa mwaka 2018/2019 ya halmashauri hiyo baada ya kufikia katika kipengele cha posho ambapo madiwani hao wameeleza kuchukizwa na taarifa za wao kutohudhuria kikao cha baraza hilo kilichofanyika tarehe 8 mwezi huu kutokana na kutokulipwa posho za vikao viwili vilivyopita.

Diwani wa viti maalum Nuru Ndosi amesema taarifa hizo zilikuwa  za udhalilishaji kwani hawakuchaguliwa na wananchi wao kwa ajili ya posho hivyo ni vema posho hizo zikafutwa ili wasiendelee kudhalilishwa.

Diwani wa kata ya Olmotonyi John Lengutai ameeleza kuwa wao hawakukataa kwenda kwenye baraza kwa ajili ya posho Bali ni kutokana na kauli ya Mkurugenzi wa halmashauri hiyo Dokta Charles Mahera aliyoitoa tarehe 6 mwezi huu kuwa anaweza  kuongoza halmashauri hiyo bila madiwani.

Aidha Mkurugenzi wa halmashauri hiyo Dokta Charles Mahera ameeleza kuwa suala la posho liko kisheria na kwamba wao wako tayari kufuta posho hizo kama madiwani wote watakubaliana ili fedha hizo zielekezwe kufanya maendeleo kwa wananchi
Share To:

msumbanews

Post A Comment: