KANUNI YA KWANZA
Panda mapema
Tayarisha shamba mapema kwa zana yoyote iliyo ndani ya uwezo wako (jembe, maksai, trekta).
Kwa wilaya ya Mbozi Panda kuanzia tarehe 15 Novemba hadi kati kati ya mwezi Desemba.
KANUNI YA PILI
Panda kwa nafasi
Mmea hadi mmea: sentimeta 30 (sawa futi moja). Weka mbegu moja kila shimo au sentimeta 60 (futi 2). Weka mbegu mbili kila  shimo.
Mstari hadi mstari: sentimeta 75 (au futi 2 na nusu). K wa wanaopenda kufuata mfereji
wa jembe la maksai inapendekezwa nafasi iwe sentimeta 90 na mbegu zidondoshwe sentimeta 25.
Usipokuwa na uhakika wa uotaji panda mbegu 2 au 3 kwa kila shimo. Yakiota yote punguza yabaki moja (au mawili) kila shimo kwa kusokota mhindi na kuvuta ili mzizi wa mmea unaobaki usidhurike.
KANUNI YA TATU
Panda mbegu bora: Kuna aina tatu za mbegu, chotara (hybrid), kompositi na kienyeji (asili).
Sehemu za miinuko ya juu (mita 1500-2300 kutoka usawa wa bahari), UH615, UH6303, TMV-2, PAN691, H625, H614D, Seedco627 nk.
Sehemu za miinuko ya kati (100-1500) UH6303, TMV-2, SC627, Staha, Kilima nk.
Nunua kilo 10 kwa kila eka, mbegu zinazobaki zitumie kurudishia ambazo hazitaota/kuharibiwa na ndege au Panya.
Nunua mbegu bora kwenye mifuko yake halisi. Pia dai risti ili uweze kuhalalisha malalamiko endapo mbegu hiyo itakuwa na matatizo baadaye.  
KANUNI YA NNE
Tumia mbolea.
Samadi/mboji: Tani 5-8 kwa ekari.
Changanya na mfuko 1 wa TSP kwa ekari. Weka mbolea kwenye shimo la kupandia au rutubisha shamba zima kwa kuifukia kwa jembe la mkono, maksai au trekta kabla ya kupanda.
Mbolea za chumvi chumvi.   
Mtiririko huu unaonyesha matumizi ya Nitrogen inayohitajika wakati wa kupanda na wakati wa kukuzia.
Sehemu zenye mvua nyingi (mm 750 au zaidi)
-SA mfuko 1 na nusu kupandia, mifuko 3 kukuzia.
-CAN mfuko 1 kupandia, mifuko 2 na nusu kukuzia.
-UREA mfuko 1  kupandia, mfuko 1 na nusu kukuzia.
-DAP mfuko 1 kupandia, SA 4, au CAN 3 au Urea 2 kukuzia.
Maeneo yenye mvua haba (mm550-750)
-SA 1 kupandia, mifuko 2 kukuzia.
-CAN 1 kupandia, mfuko 1 na nusu kukuzia.
-UREA nusu mfuko kupandia, mfuko 1 na nusu kukuzia.
-DAP 1 kupandia, SA 4 NA nusu au CAN 3 au Urea 1 kukuzia.
Katika maeneo yenye mvua chini ya mm 550 kwa msimu ni lazima umwagiliaji ufanyike.
KANUNI YA TANO
Palilia vizuri.
Palilia mahindi mara 2 au 3, palizi ya kwanza iwe wiki 2-3 baada ya mbegu kuchipua. Ya pili au tatu baada ya mbegu kuchanua. Uzaaji hauongezeki ukipalilia baada ya mhindi kuchanua. Kwa wenye uwezo zipo dawa za kuua magugu (mfano PRIMAGRAM, ATRANEX, GESAPRIM, GRAMAXONE, ROUNDUP nk)
KANUNI YA SITA
Zuia wadudu waharibifu (hasa bungua)
Nyunyizia dawa kwenye majani ya mahindi yakiwa na urefu wa sm75, rudia baadae ukiona mashambulizi.

Dawa za viwandani:
 Actellic, Thionex, Endosulfan, Dursban, Karate, Dimepaz 40 na nyinginezo.Kipimo: mls 30 kwa lita 15 za maji.
Dawa za asili: kwa mfano utupa, dawa hizi hazina kiwango maalumu.
NB: Mbegu bora za mahindi zina uwezo wa kustahimili magonjwa ya mahindi.
KANUNI YA SABA
Hifadhi vizuri kwenye mifuko, ghalani au mapipa.
Hakikisha sehemu hizo ni kavu, safi, dawa za kuua wadudu zimepulizwa maeneo hayo. Actellic EC 50 ya maji inafaa sana kudhibiti wadudu wa ghalani.
Mkulima, zingatia kanuni za uzalishaji bora wa Mahindi ili kuongeza kipato.
Share To:

msumbanews

Post A Comment:

Back To Top