Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama (JWTZ), Jenerali Venance Mabeyo amewataka Watanzania kujiepusha na vitendo vinavyoweza kutishia usalama wa nchi na kuharibu tunu ya amani iliyopo.

Ameeleza kuwa hivi sasa vipo viashiria vinavyotishia usalama wa nchi, na kwamba hatua zinachukuliwa ili kudhibiti hali hiyo.

Jenerali Mabeyo amewaomba Watanzania kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Rais John Magufuli dhidi ya wizi, ufisadi na matumizi mabaya ya ofisi za umma, kwa kuwataja hadharani watu wanaojihusisha na vitendo hivyo.

Ametoa kauli hiyo jana wakati akifunga Maadhimisho ya Tamasha la Mashujaa wa Vita ya Majimaji katika Viwanja vya Makumbusho ya Mashujaa wa Vita ya Majimaji mjini Songea.

Mabeyo amesema vita dhidi ya wizi na ufisadi, iliyoanzishwa na Rais Magufuli, si ya mtu mmoja, bali kila Mtanzania anapaswa kushiriki, kwani mali zinazoibwa na baadhi ya Watanzania, zinapaswa kuwanufaisha watu wote.

Mabeyo alisema badala ya kushughulika na uvunjifu wa amani, ipo haja ya Watanzania kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, ambayo imedhamiria kuwatumikia wananchi kwa kuboresha huduma za kijamii ili kutoa fursa kwa wananchi kutumia muda wao kufanya kazi za kujiletea maendeleo.

Ametaja baadhi ya mambo yanayotishia usalama wa nchi kuwa ni matumizi mabaya ya utandawazi ambayo mbali na ya kuharibu utamaduni wa nchi, baadhi ya watu wanaitumia vibaya kwa kuhamasisha wananchi kufanya na kushiriki katika matukio ambayo yanaashiria uvunjifu wa amani na utulivu uliopo nchini kwa muda mrefu.

Jenerali Mabeyo alitaka shule za msingi, sekondari na vyuo nchini, kufundisha wanafunzi umuhimu wa kulinda, kutunza amani na wananchi kuishi kwa kupendana, badala ya kutumia muda wao kutafuta sababu za kutengana, jambo ambalo halina tija kwa taifa.

Wakati huo huo, Jenerali Mabeyo aliitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kuboresha Makumbusho ya Mashujaa wa Vita ya Majimaji ili yatumike kwa ajili ya utalii na kuliingizia taifa fedha nyingi.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Chiristina Mndeme alisema Serikali ya Mkoa wa Ruvuma, itaongeza nguvu katika kulinda mipaka yake ili wananchi wa mkoa huo waweze kuendelea na kazi za uzalishaji mali.
Share To:

msumbanews

Post A Comment: